2012-11-28 10:40:16

Mawaziri wa mambo ya ndani ya nchi wanajadili mkakati wa kufuta Adhabu ya Kifo! Hakuna haki pasi na maisha!


Jumuiya ya Mtakatifu Egidio imeandaa Kongamano la Saba la Kimataifa linalowashirikisha Mawaziri wa Mambo ya ndani ya nchi kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wanaojadili kuhusu adhabu ya kifo, kwa kuongozwa na kauli mbiu "Dunia pasi na adhabu ya kifo; hakuna haki pasi na maisha".

Haki na maisha na dhana zinazokwenda sanjari, changamoto kwa wanasiasa wanatekeleza dhamana hii katika sera na mikakati yao kuhusu utekelezaji wa misingi ya haki ndani ya Jamii. Hadi sasa kuna nchi 150 ambazo zimefuta katika sheria zake utekelezaji wa adhabu ya kifo, kama kielelezo cha kutaka kuenzi haki msingi za binadamu.

Wataalam wanabainisha kwamba, adhabu ya kifo ni kielelezo cha hali ya juu cha uvunjaji wa haki msingi za binadamu; jambo ambalo linakwenda sanjari na ubaguzi unaofanywa katika mifumo mbali mbali ya maisha ya binadamu. Idadi kubwa ya watu wanaohukumiwa adhabu ya kifo ni maskini! Watu wenye fedha zao, wanaweza kujitetea na hatimaye kuepuka adhabu ya kifo, lakini maskini, watakiona cha mtema kuni.

Takwimu nchini Marekani ambako adhabu ya kifo inaendelea kutekelezwa zinaonesha kwamba, kati ya kesi 15,978; wazungu wapatao 30 tu ndio waliohukumiwa kunyongwa hadi kufa, wakati ambapo 15948 kutoka katika makundi mbali mbali walipatikana na hatia ya kunyongwa hadi kufa! Kuna makosa ya kisheria yanayofanyika na matokeo yake watu wasiokuwa na hatia wanajikuta wamenyongwa na haki yao kupotea kabisa.

Bi Theresa Makone anasema, nchini Zimbabwe, adhabu ya kifo haijawahi kutekelezwa kwa kipindi cha miaka 32, hali inayoonesha kwamba, kuna haja ya kufanya marekebisho ya sheria ili kufuta adhabu ya kifo nchini humo. Falsafa ya jicho kwa jicho ni hatari kwani nchi inaweza kujikuta ikiwa na vipofu wengi. Kwa hakika, adhabu ya kifo ni kitendo kinachopingana na utu wema pamoja na haki msingi za binadamu.

Hiki ni kielelezo cha watu kutaka kulipizana kisasi, jambo ambalo kamwe halina tija wala maendeleo kwa Jamii husika. Kutokana na changamoto hizi, kuna haja kwa Wanasiasa na Jamii kwa ujumla, kusimama kidete kupinga adhabu ya kifo, kwani Jamii haiwezi kuongozwa kwa msingi wa hofu na kwamba, magereza yamekuwa ni maeneo ya taabu na mahangaiko ya watu wengi wasiokuwa na hatia, jambo ambalo haliwezi kuvumilika. Kuna haja ya kutafuta njia mbadala dhidi ya adhabu ya kifo!







All the contents on this site are copyrighted ©.