2012-11-28 08:46:03

Kardinali Polycarp Pengo anawahimiza Wanawake Wakatoliki kumwilisha upendo kwa vitendo!


Ifuatayo ni hotuba ya Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, wakati wa uzinduzi wa maonesho ya Wanawake Wakatoliki Tanzania, yaliyofanyika hivi karibuni Jimbo kuu la Dar es Salaam, kama sehemu ya kumbu kumbu ya miaka 40 tangu WAWATA ilipoanzishwa.

Mhashamu Askofu Mkuu Francisco M.Padilla Balozi wa Baba Mtakatifu Nchini Tanzania.
Mhashamu Askofu Desiderius Rwoma –Mwenyekiti wa Idara ya Utume wa Walei katika Baraza la Maasfofu Katoliki Tanzania.
Waheshimiwa Mapadre, Watawa wa kike na wakiume
Waheshimiwa Viongozi Mbalimbali wa Serikali na Taasisi
Wageni Waalikwa toka Kenya, Uganda, Malawi na Zambia
Wapendwa mama zangu WAWATA.

Adhimisho la Miaka 40 ya WAWATA ni tendo ambalo limelifurahisha sana Kanisa katika ngazi zote kwa sababu limetoa fursa ambapo WAWATA kwa namna ya pekee mumeweza kutafakari Utume wenu katika kanisa na jamii hasa mkijikita katika kauli mbiu ya adhimisho la miaka 40 ya WAWATA “Upendo kwa Vitendo”Katika harakati zenu za ujumla za kutumikia kwa Upendo wa Kristu.

Kanisa zima la Tanzania linawapongeza sana kwa hatua mliyofikia na kuwaasa kwamba tafakari mlizofanya katika ngazi zote kwa kipindi chote ziwe chachu ya kuongeza juhudi na kuwajibika zaidi awamu nyingine za miaka ijayo baada ya adhimisho hili.

Nimefurahishwa binafsi na kujifunza mengi sana kutokana na maonesho ambayo mmenipa fursa ya pekee ya kuyafungua. Nimejionea mwenyewe mambo mbalimbali ambayo ni vielelezo vya kazi ya Mwanamke Mkatoliki katika nyanja za kujiendeleza kiroho na kimwili hususani ; Uchumi, malezi ya watoto na vijana , utunzaji wa, mazingira, elimu ya dini n.k kwa kuzingatia Kauli mbiu ya WAWATA ya “Kwa Upendo wa Kristu Tutumikie na Kuwajibika”

Mnafanya kazi nzuri ambazo ni kwa ajili ya maendeleo ya kanisa na jamii kwa ujumla. Umoja wenu unajitahidi kuwafanya WAWATA wajitakatifuze; ili waweze kuyatakatifuza malimwengu kazi ambayo kwa ubatizo wenu mmeitwa kufanya. Ushiriki wenu katika Jumuiya Ndogo Ndogo za Kikristo ni muhimu sana katika kuyatakatifuza malimwengu kwani kwa kupitia Jumuiya Ndogo ndogo zinazowajibika ,ndipo tunapata familia bora zenye kutoa viongozi bora wa kanisa na taifa.

Munashiriki harakati mbalimbali za kujikomboa kiuchumi k.m: kuondokana na umaskini,unyanyasaji, maradhi ili kwa kujikomboa kwenu muwakomboe wengine na kuwa chachu ya maendeleo kuanzia ngazi ya familia hadi taifa . Kanisa limeshuhudia mkianzisha na kutekeleza miradi mbalimbali katika vikundi vyenu, vigango, parokia majimbo, n.k. Uongozi unaowajibika,na uaminifu katika kutekeleza hayo yote ni muhimu sana ili shughuli hizo zote ziwe endelevu na kuleta mabadildiko yenye kuwanufaisha walengwa na jamii kwa ujumla.

Aidha nimefurahi sana kuona mmetenga muda wa kujadili na kutoa maoni yenu kuhusiana na marekebisho katiba ya Jamhuri Muungano wa Tanzania. Ni jambo Muhimu sana kwani ni wajibu wenu kufanya hivyo hivyo nawahimiza mushiriki kikamilifu mchakato huo katika ngazizake zote .

Mnapotafakari kauli mbiu ya “Upendo kwa Vitendo” Mnafahamu Yesu Kristo mwenyewe alitudhihirishia Upendo wa Mungu kwa maisha yake yote. Ndiyo maana alisema: “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake”. (Yohane 15:13.) Alionyesha haya katika kuwafundisha wafuasi wake kwa hali na mali. Aliwaponya wagonjwa, viwete vipofu, viziwi na bubu n.k. Aliona shida za watu akajali na kuwajibika katika kuwahudumia bila kutafuta faida.

Dunia ya leo inahitaji sana upendo ili amani na ustawi viweze kushamiri. Hivyo WAWATA na wanawake kwa ujumla ambao ni wa kwanza katika dhamana ya uhai wa bianadamu wana nafasi ya pekee katika jamii.Hivyo natoa mwito kwa dhati kabisa kuwa pandeni mbegu za upendo kwanza katika familia iliyo shule ya kwanza ili watoto wote waonje upendo wa baba na mama na hivyo waweze kuiga na kuwa raia wema. Hivyo mtakapondaa mkakati wa shughuli za WAWATA katika kipindi kijacho.

Zingatieni sana malezi yenye kujenga upendo katika familia ili kizazi kijacho kiwe na amani na ustawi zaidi .Mwito huu ni kwa ajili ya wazazi wote yaani baba na mama pamoja na wale wote wanaohusika na malezi ya wataoto na vijana katika jamii zetu walezi .Tuonyeshe Upendo kwa vitendo ili kwa matendo yenu jamii iwatambue kuwa nyinyi ni wafuasi kweli wa Kristu!

Nawapongeza sana kwa maadhimisho haya ya miaka 40 ya Umoja wenu WAWATA na nawatakia heri na baraka katikasafari ya kuelekea mbele yenye kujituma zaidi.

“Kwa upendo wa Kristo,Tutumikie na Kuwajibika”

Asanteni sana

Polycarp Kardinali Pengo.









All the contents on this site are copyrighted ©.