2012-11-27 08:22:08

Majaji wa Mahakama kuu waapishwa Ikulu, Dar es Salaam


Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatatu, Novemba 26, 2012 amewaapisha Majaji wawili wa Mahakama Kuu ya Tanzania kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania. Katika sherehe iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Jaji Mkuu, Mheshimiwa Mohamed Chande Othman, Rais Kikwete amewaapisha Jaji Bethuel M.K. Mmilla na Jaji Ibrahim Juma kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani.

Rais Kikwete aliwateua Majaji hao tokea Oktoba 25, mwaka huu wa 2012, na kabla ya uteuzi wake, Jaji Bethuel M.K. Mmilla alikuwa Jaji wa Mahakama Kuu kwa miaka kumi tangu Juni 02, 2002. Vile vile, Jaji Mmilla amekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kwenye vituo vya Sumbawanga, Arusha na Mbeya.

Naye Jaji Ibrahim Juma kabla ya uteuzi wake alikuwa Mwenyekiti wa Tume ya Kurekebisha Sheria tangu mwaka 2007 na pia Jaji wa Mahakama Kuu tangu Juni, 2009. Pia amewahi kuwa Mkuu wa Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kati ya mwaka 2003 na mwaka 2006.

Wakati huo huo, Rais Kikwete amemwapisha Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mheshimiwa John Mkwawa kuwa Mjumbe wa Tume ya Uchaguzi ya Taifa (NEC) na amemwapisha Bi. Winfrida Beatrice Korosso kuwa Katibu wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania.








All the contents on this site are copyrighted ©.