2012-11-27 08:29:32

CAFOD inaadhimisha Jubilee ya miaka 50 kielelezo cha mshikamano wa upendo


Shirika la Misaada na Maendeleo Kimataifa la Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza, CAFOD linaadhimisha Jubilee ya miaka hamsini tangu lilipoanzishwa, kielelezo makini cha mshikamano wa upendo unaoongozwa na kanuni auni kwa watu wanaokabiliwa na shida mbali mbali duniani.

Shirika hili lilianzishwa kunako mwaka 1962 wakati wa vugu vugu la maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Waamini na watu wenye mapenzi mema, wakaalikwa kwa namna ya pekee na Kanisa kufunga na kujinyima wakati wa kipindi cha Kwaresima, ili kile kidogo walichojinyima, kiweze kukusanywa na kupelekwa katika maeneo yaliyokuwa yanahitaji msaada zaidi.

Kunako mwaka 1967 Papa Paulo wa sita, akaandika Waraka wa Kichungaji: Maendeleo ya Watu, Populorum Progressio. Waraka huu kwa miaka yote hii, umekuwa ni dira na mwongozo wa maisha na utume wa CAFOD sehemu mbali mbali za dunia. Mang’amuzi yake yameboreshwa zaidi na Nyaraka nyingine zilizotolewa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili: Sollicitudo rei socialis na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Upendo katika Ukweli.

Hili ni Shirika la misaada ambalo kimsingi linaongozwa na Imani ya Kanisa Katoliki inayofafanuliwa katika Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki na Mafundisho Jamii ya Kanisa. Kwa kipindi cha miaka hamsini, CAFOD imeshikamana na wadau mbali mbali wa maendeleo kutoka Afrika, Asia na Amerika ya Kusini, ili kukabiliana na majanga asilia, maafa na athari za vita, kinzani na migogoro.

Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, zaidi ya Sterling za Uingereza Milioni arobaini na tatu zimetumika kwa ajili ya kugharimia misaada ya maendeleo sehemu mbali mbali za dunia pamoja na kukabiliana na majanga asilia na maafa mbali mbali. Ni utume ambao unatekelezwa kwa kuwahusisha watoto na vijana ambao wanajinyima ili kuchangia ustawi na maendeleo ya watu wanaokabiliana na umaskini, ujinga na maradhi.

Huu ni utamaduni wa upendo na mshikamano, unaojitahidi kumwilisha Injili ya Upendo, kwa kuguswa na mahitaji ya jirani. Kwa maneno mengine, hii ni imani katika matendo, inayopania kujenga Ufalme wa Mungu hapa duniani. Mikakati yake ya maendeleo inamlenga mtu mzima: kiroho na kimwili, kwani wanatekeleza wajibu na dhamana hii kwa kuhakikisha kwamba, wanajikita katika kumletea mwanadamu maendeleo endelevu na ya kudumu.

Katika kipindi cha miaka hamsini iliyopita, mengi yamefanyika hususan katika sekta ya afya, elimu, maendeleo endelevu, kilimo, uchumi. Wameendelea kuzihimiza Serikali kusimamia utawala bora sanjari na kufuta deni la nje, ambalo kwa nchi nyingi limekuwa ni kikwazo cha maendeleo endelevu. CAFOD katika mikakati yake, inapania kusimama kidete dhidi ya umaskini na ukosefu wa misingi ya haki jamii, daima wakiongozwa na Kweli za Kiinjili, kwani haya ni kati ya mambo yanayotiliwa mkazo katika majiundo ya wafanyakazi na wanachama wa CAFOD.

Jubilee ya Miaka hamsini ya CAFOD ni kipindi muafaka cha kuweza kufanya tathmini ya kina, kumshukuru Mungu kwa wema na ukarimu aliowatendea pamoja na kuomba ulinzi na salama kutoka juu mbinguni, ili waendelee kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya maendeleo endelevu kwa watu wanaoogelea katika baa la umaskini, ujinga na maradhi.

CAFOD kwa sasa inakabiliwa na changamoto nyingi kati ya hizi ni myumbo wa uchumi kimataifa na athari zake kwa mamilloni ya watu sehemu mbali mbali za dunia; athari za mabadiliko ya tabianchi; njaa, ukame pamoja na majanga asilia. Haya ni mambo yanayodumaza maendeleo ya watu. Jubilee ya miaka hamsini ya CAFOD ni mwaliko wa kusimama kidete kupambana na changamoto zote hizi, ili hatimaye, kujega misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kimataifa unaoongozwa na kanuni auni.

Mwaka wa Imani, uwe ni kipindi muafaka wa kuonesha Imani katika matendo, ili kwamba, kila mtu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu aweze kuheshimiwa na kuthaminiwa utu wake.








All the contents on this site are copyrighted ©.