2012-11-24 09:16:39

Waamini wa Kanisa Katoliki Afrika ya Kaskazini ni wachache lakini: ni mashahidi wa majadiliano, huduma, sala na mang'amuzi mbali mbali ya maisha!


Baraza la Maaskofu Katoliki Kanda ya Afrika ya Kaskazini, CERNA, limehitimisha mkutano wake wa mwaka, uliofanyika Jimboni Mazara del Vallo, Sicilia, Kusini mwa Italia, kwa mwaliko wa Askofu Domenico Mogavero.

Maaskofu hao wamekazia umuhimu wa kuendeleza na kudumisha majadiliano ya kitamaduni kwa watu wanaoishi katika Ukanda wa Mediterrania; kinzani na migogoro inayoendelea kuhatarisha haki, amani na usalama huko Mashariki ya Kati, tatizo la uhamiaji na misimamo mikali ya kidini; mambo ambayo yanapaswa kuangaliwa kwa umakini mkubwa, kwa ajili ya maendeleo na ustawi wa wananchi wa Afrika ya Kaskazini.

Maaskofu wanatambua kwamba, Waamini wa Kanisa Katoliki ni wachache Kaskazini mwa Afrika, lakini ni kielelezo makini cha ushuhuda, majadiliano ya kina, huduma, maisha ya sala na mang'amuzi mbali mbali yanayopata chimbuko lake kutoka katika eneo hili. Maaskofu wamejadili na kutoa mwongozo wa kukabiliana na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya watoto wadogo, bila kusahau tatizo la wahamiaji ambalo linaendelea kuongezeka siku hadi siku kutokana na kinzani na vita huko Mashariki ya Kati.

Makanisa ya Kaskazini mwa Afrika yana idadi kubwa ya waamini wahamiaji wanaotoka Kusini mwa Jangwa la Sahara kwa sababu mbali mbali, lakini wengi wao ni wale ambao wako njiani kuelea Ulaya kupitia Sicilia. Ni kundi la watu wanaokabiliana na changamoto na hali ngumu katika maisha yao, anasema Askofu Domenico Mogavero.

Tofauti za kidini na kitamaduni zisiwe ni sababu ya choko choko na kinzani za kijamii, bali utajiri unaowawezesha watu kuvumiliana, kushirikiana na kutolea ushuhuda wa tunu msingi za kijamii na kidini zinazowaunganisha badala ya kila upande kung'ang'ania na kuendelea kushikilia mambo madogo madogo yanayowagawanya!

Bado kuna ubaguzi unafanywa kwa misingi ya kidini, kwani kwa Wakristo wanaoishi Kaskazini mwa Afrika wanadhaniwa kwamba, ni raia wa daraja la pili na hawana haki sawa na wananchi wengine wenye imani tofauti na ile ya kwao. Ubaguzi huu unafanyika hata katika sheria za nchi, kwani hakuna uhuru wa dhamiri.







All the contents on this site are copyrighted ©.