2012-11-24 08:51:58

Chuo Kikuu cha Dodoma kinavyojipanga kupunguza gharama za matibabu ya ugonjwa wa figo!


Rais Mstaafu wa awamu ya Tatu, Benjamin William Mkapa, ameishauri Serikali kupanga utaratibu utakaosaidia wagonjwa wa figo kumudu gharama za matibabu pindi huduma hiyo itakapoanza kutolewa Januari mwakani na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Mkapa ametoa ushauri huo Ijumaa tarehe 23 Novemba 2012, wakati alipotembelea chuo hicho, kukagua mashine za kisasa 10 za kusafisha damu zilizotolewa na Serikali ya Japan kupitia Mfuko wa Benjamin. Amesema, kutokana na uchumi walionao Watanzania wa kawaida hawataweza kumudu kulipia gharama za matibabu hizo kwa kuwa ni ghali sana .

Kwa kuwa hospitali zinazotoa matibabu hayo hapa nchini ni chache hivyo hospitali hiyo ijiandae kuwapokea wangonjwa wengi kutoka ndani ya nchi na nje ya nchi. Akizungumzia kuhusiana na msaada wa mashine hizo, Mkapa amesema awali taasisi yake iliomba msaada wa mashine hizo kutoka Japan kwa ajili ya kufundishia wanafunzi wa Chuo Kikuu hicho ili waweze kujifunza kuwatibu wagonjwa hao. Hata hivyo, amesema kutokana na mahitaji ya chuo hicho wamebaini ni vema wakaongeza idadi ya wataalam hao.

Naye Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Noah Chihoma, amesema Chuo hicho kilipeleka wafanyakazi sita nchini Japan kujifunza jinsi ya kutumia mashine hizo za kisasa za kusafisha damu. Dk. Chihoma amesema kwa sasa mashine hizo hazijaanza kutumika kwa sababu bado wanasubiri wataalamu wa kutoka kampuni nchini Japan ili waweze kufanya uhakiki wa mwisho ili zianze kutumika.

Amesema pamoja na wataalamu hao sita kutoka hospitali yao, watashirikiana na wataalamu wengine kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ili kuweza kuziendesha mashine hizo. Dk. Chihoma amesema kwa sasa hivi hospitali yao pamoja na kutibu magonjwa ya kawaida kwa wafanyakazi na wanafunzi, pia kinatoa matibabu kwa Jamii inayokizunguka chuo hicho.








All the contents on this site are copyrighted ©.