2012-11-21 08:31:19

Siku ya Wavuvi Duniani 21 Novemba 2012


Takwimu za kimataifa zinabainisha kwamba, kuna jumla ya wafanyakazi milioni thelathini, wanaotekeleza wajibu wao katika sekta ya uvuvi sehemu mbali mbali duniani. Lakini hii ni sekta ambayo inasemekana kuwa ni hatari sana, ikilinganishwa na kazi nyingine zozote, kwani wavuvi wamekuwa wakikumbana na nyanyaso, dhuluma na ma teso ya kila aina, wanapotekeleza wajibu wao, ili kuhakikisha kwamba, mamillioni ya watu wanapata samaki safi na salama kwa ajili ya kitoweo.

Inakadiriwa kwamba, asilimia kumi na tatu ya wavuvi wote duniani ni watu wanaokabiliana na hatari kubwa zaidi katika maisha yao. Hali hii ni mbaya zaidi katika nchi zinazoendelea duniani, kwani wanakabiliwa na hatari kubwa ya kifo, ikilinganishwa na wavuvi kutoka katika nchi zilizoendelea zaidi duniani.

Yote haya yanajadiliwa kwa namna ya pekee na wajumbe wanaohudhuria Kongamano la ishirini na tatu la kimataifa la Utume wa Bahari lililoandaliwa na Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, inayoendelea hapa mjini Vatican. Itakumbukwa kwamba, kila mwaka ifikapo targhe 21 Novemba, Jumuiya ya Kimataifa inaadhimisha Siku ya Wavuvi Duniani.

Lengo la Utume wa Bahari ni kuhakikisha kwamba, hata ulimwengu wa mabaharia unashiriki kikamilifu katika dhamana ya Uinjilishaji Mpya; changamoto endelevu inayofanyiwa kazi na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Mwakilishi wa Shirika la Kazi Duniani, ILO amezungumzia kuhusu Mkataba wa Shirika hilo namba 188 unaozungumzia kuhusu sekta ya uvuvi duniani. Jambo la kusikitisha ni kuona kwamba, hadi leo hii, Mkataba huu haujapata idadi kubwa ya nchi wanachama wa Shirika la Kazi Duniani wanaouunga mkono, kiasi cha kushindwa kutekelezwa na nchi wanachama. Wanachama wa Utume wa Bahari kwa kushirikiana na watu wanaojitolea wanaendelea kuzihamasisha nchi wanachama wa ILO, kuridhia Mkataba huu, ili uweze kuwa ni sheria.

Sekta ya uvuvi imegawanyika katika makundi makuu matatu: uvuvi wa kujikimu, uvuvi wa soko mahalia na uvuvi wa kimataifa. Wajumbe kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wametoa ushuhuda unaonesha utawala bora katika sekta ya uvuvi sanjari na kulishirikisha Kanisa katika maisha na utume wa wavuvi, jambo ambalo bado liko nyuma sana kwa nchi nyingi za Kiafrika. Lakini, ikumbukwe kwamba, ni kundi ambalo linakabiliana na hatari kubwa katika maisha yake, hivyo linapaswa kupewa kipaumbele cha pekee katika maisha na utume wa Kanisa kwa kukazia Utume wa Bahari mahali ambapo bado haujaanzishwa.

Kutoka nchini Angola, Utume wa Bahari unaonesha kuzaa matunda mazuri kutokana na ushirikiano uliopo kati ya Kanisa na Jumuiya ya Wavuvi wanaoishi Angola na Sao Tomè. Wanaendelea kuandamana na Jumuiya ya wavuvi katika mahitaji yao ya kijamii na kiroho pamoja na kujiunga nao wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wavuvi, ili kutambua kwamba, Kanisa linawathamini na linataka kuwaenzi, licha ya changamoto na kinzani mbali mbali wanazokabiliana nazo katika utume wao. Utume wa Bahari umekuwa ni msaada mkubwa katika mapambano dhidi ya Ukimwi, matumizi haramu ya dawa za kulevya pamoja na ulevi wa kupindukia.

Wahamasishaji wa kongamano hili wanasema kwamba, hata wavuvi wanapaswa kutangaziwa Habari Njema ya Wokovu, kwa kuzinagatia: mazingira na mahitaji ya watu wanaofanya kazi katika sekta ya uvuvi. Wafundishwe Biblia, Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki na Mafundisho Jamii ya Kanisa bila kusahau maisha ya Sala na Sakramenti za Kanisa. Familia za wavuvi zisaidiwe kukabiliana na changamoto za maisha kwa imani na matumaini. Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, yatoe changamoto kwa Mama Kanisa kuwawezesha wavuvi kuzima kiu ya maisha yao ya kiroho.








All the contents on this site are copyrighted ©.