2012-11-21 08:38:08

Mwaka wa Imani uimarishe Imani kwa Kristo na Kanisa lake!


Kardinali John Njue, Askofu mkuu wa Jimbo Kuu la Nairobi, hivi karibuni wakati wa maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, kwa ajili ya Mashirika ya Kipapa ya Utoto Mtakatifu, amewaalika waamini nchini Kenya kuhakikisha kwamba, wanatumia vyema maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ili kuimarisha imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.

Kardinali Njue anasema, Mwaka wa Imani ni kipindi cha neema na wakati uliokubalika kwa waamini kuweza kuimarisha imani, matumaini na mapendo. Huu ni utume endelevu wa Mama Kanisa ambao kila mwamini anapaswa kuushiriki kikamilifu. Dhamana hii fungamanishi, inapaswa kujikita kuanzia ndani ya familia za kikristo, kwenye Jumuiya ndogo ndogo, vyama vya kitume na Kanisa katika ujumla wake.

Katika Ibada hii ya Misa Takatifu Watoto wa Utoto Mtakatifu kutoka katika Parokia kumi na moja zinazounda Jimbo kuu la Nairobi, walijumuika kusali kwa pamoja, kwenye Parokia ya Bikira Maria Malkia wa Amani, iliyoko Kusini mwa Nairobi. Kardinali Njue anawataka viongozi wa Kanisa kutumia Ibada mbali mbali za Kanisa kwa ajili ya kuimarisha Imani yao.

Kwa namna ya pekee, anawaalika Makleri, Watawa, Makatekista na Wazazi kuhakikisha kwamba, wanakuwa ni chumvi na mwanga wa Imani kwa wote wanaowahudumia. Wajitahidi kuhakikisha kwamba, watoto wanapewa kipaumbele cha pekee kama sehemu ya mchakato wa kurithisha imani ya Kristo na Kanisa lake kwa watoto hawa ambao kimsingi ni jeuri na tumaini la Kanisa imara na thabiti kwa sasa na kwa siku za usoni.








All the contents on this site are copyrighted ©.