2012-11-21 11:34:45

"Majembe" ya Uongozi wa Shirika la Masista wa Ivrea yakamilika!


Shirika la Masista wa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili la Ivrea, hivi karibuni lilihitimisha maadhimisho ya mkutano wake wa thelathini na tano kwa kumchagua kwa mara nyingine tena Mheshimiwa Sr. Palma Porro, kuwa Mama Mkuu wa Shirika kwa kipindi kingine cha miaka sita. RealAudioMP3

Kabla ya kuchaguliwa kwa mara ya kwanza kuliongoza Shirika, Sista Palma Porro alikuwa anafanya utume wake nchini Tanzania kama mmissionari na mlezi wa Wanovisi, katika nyumba yao ya Malezi iliyoko Miyuji, Jimbo Katoliki la Dodoma.

Katika utume wake wa kuliongoza Shirika, atashirikiana kwa karibu zaidi na Washauri wake wakuu kama ifuatavyo: Sr. Anna Mastropasqua; Sr. Salome Aoko Odongo, kutoka Kenya, ambaye pia amechaguliwa kwa mara ya pili katika nafasi hii. Wengine ni Sr. Donatela Gareffa pamoja na Sr. Franca Pavin.

Shirika la Masista wa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili la Ivrea, linafanya utume wake sehemu mbali mbali duniani. Barani Afrika wamejikita zaidi nchini Libya, Kenya na Tanzania.

Mheshimiwa Sr. Palma Porro, Mama Mkuu wa Shirika la Masista wa Ivrea, katika barua yake kwa Masista wenzake, anawaalika kwa namna ya pekee wawe ni chumvi ya dunia na mwanga wa mataifa, kauli mbiu ambayo iliongoza maadhimisho ya Mkutano mkuu wa thelathini na tano wa Shirika.

Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita hivi karibuni, ni mwaliko kwa Watawa wa Ivrea kumwongokea Mwenyezi Mungu, kwa kujitahidi kumfahamu zaidi Yesu Kristo, ili kuboresha uhusiano wa kibinadamu kwa kujikita zaidi katika mchakato wa mshikamano na udugu.

Masista wa Ivrea wanatambua umuhimu wa Imani kama nguvu inayoleta mabadiliko ya ndani kwa kuwa makini katika mustakabali wa maisha yao kwa siku za usoni, ukweli wa wito wao katika historia, maana ya maisha na kwamba, wao ni wasafiri kuelekea Yerusalemu ya mbinguni.

Mheshimiwa Sr. Palma anasema kwamba, mara baada ya maadhimisho ya Mkutano Mkuu wa Shirika, Masista wameendelea kusali na kusubiri kwa hamu ili kufahamu majina ya wale waliopewa dhamana ya kuliongoza Shirika katika Kanda mbali mbali.

Ni kipindi ambacho wamekuwa wazi kusikiliza sauti ya Roho Mtakatifu, wakafanya hija ya Imani, kwa kutambua changamoto na fursa mbali mbali zilizoko mbele ya Shirika na hatimaye, kuchagua watu ambao watawasaidia watawa wenzao kuendelea na hija ya uaminifu kwa wito wao wa kitawa, karama ya Shirika, lakini zaidi kwa kuwa ni waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake.

Anawashukuru kwa namna ya pekee, Masista waliokuwa wamepewa dhamana ya kuliongoza Shirika kwenye Kanda mbali mbali, kwa mfano Mheshimiwa Sr. Raffaela Franzin aliyekuwa Mama Mkuu wa Kanda ya Malaika Mkuu Mikaeli, inayowaunganisha Masista wa Ivrea wanaotekeleza utume wao Barani Afrika.

Shirika limemchagua Mheshimiwa Sr. Enrica Agostina Giani kuwa Mama mkuu wa Kanda ya Malaika Mkuu Mikaeli. Wengine waliochaguliwa ni pamoja na:
Sr. Jenipher Muga atakayekuwa Mama mkuu msaidizi wa Kanda.
Sr. Assunta Malamso, Mshauri na Katibu wa Kanda.
Sr. Rosalia Henry, Mshauri.
Sr. Adolfina Wambua, Mshauri
Na Sr. Maria Rosaria Balestrucci, Mweka hazina wa Kanda.

Mheshimiwa Sr. Enrica Agostina Giani na Washauri wake wanatarajiwa kusimikwa rasmi hapo tarehe 16 Desemba 2012, Veyula, Jimboni Dodoma, Tanzania. Tukio ambalo litasimamiwa na na Mheshimiwa Sr. Salome Aoko, Mshauri wa Shirika, kutoka Makao Makuu, Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.