2012-11-21 08:37:42

Chama cha waamini walei wa Don Orione chatambuliwa rasmi


Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume, tarehe 20 Novemba 2012 limeandika Hati inayotambua Chama cha Waamini Walei wa Don Orione, kuwa ni kati ya vyama vya walei vinavyotambuliwa rasmi na Mama Kanisa katika maisha na utume wake.

Hili ni tukio ambalo linendelea kuongeza furaha na matumaini kwa Shirika la Mabinti wa Neema ya Mungu, lililopitishwa na Vatican kunako tarehe 20 Novemba 1954. Ilikuwa ni tarehe 6 Machi 1965 Shirika la Masista Wadogo wa Huruma lilipoidhinishwa na tarahee 13 Mei 1997 Shirika la kitume la Orionino lilipitishwa pia.

Tukio hili la kihistoria limeshuhudiwa na Kardinali Joao Braz de Aviz, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume pamoja na Mheshimiwa Padre Flavio Peloso, Mkuu wa Shirika la Kazi za Don Orione pamoja na wakuu wengine wa Chama cha Waamini Walei wa Don Orione.

Kikatiba sasa waamini hawa wataweza kushiriki karama na tasaufi ya Shirika la Don Orione kikatiba baada ya kutambuliwa rasmi na Mama Kanisa. Hili ni kundi ambalo limekuwa likiandamana bega kwa bega na Wamissionari wa Don Orione katika maisha na utume wao na kwamba, wao ni matunda ya maadhimisho baada ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Ilikuwa ni Mwaka 1992, takribani miaka ishirini iliyopita, wakati wa maadhimisho ya Mkutano mkuu wa Shirika, Chama cha Waamini Walei wa Don Orione walipowaomba wajumbe kutunga Katiba pamoja na kuanza mchakato wa kuratibu shughuli za Chama hiki na matunda ya jitihada hizi kwa sasa yameanza kuonekana, hili ni jambo la kumshukuru Mwenyezi Mungu.

Chama hiki kimeenea katika nchi thelathini, changamoto ya kuendelea kukikuza kwa kuwashirikisha walei, watawa na makleri katika maisha na utume wao.










All the contents on this site are copyrighted ©.