2012-11-20 11:28:53

Mmeimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara, sasa mnatumwa ulimwenguni ili kumshuhudia Kristo na Kanisa lake kwa ujasiri mkubwa zaid!


Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Dodoma, mapema juma hili ametembelea Parokia ya Bikira Maria Malkia wa Damu Azizi ya Yesu, Kisasa na kutoa Sakramenti ya Kipaimara kwa Wakristo sabini wa Kigango cha Mtakatifu Anna.

Katika mahubiri yake, Askofu Nyaisonga anawataka Wakristo wote kutambua dhamana na jukumu lao katika maisha na utume wa Kanisa, kwani wanahamasishwa kujikita katika umoja na mshikamano, furaha na upendo mkamilifu; daima wakijitahidi kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, kwa njia ya kuwatangazia wengine Habari Njema ya Wokovu, inayojikita katika maisha yao ya kila siku.

Shida na magumu ni sehemu ya mchakato wa hija ya maisha ya mwanadamu, lakini mambo haya yasiwafanye waamini kushindwa kuishi kwa furaha na matumaini. Wanahimizwa na Kanisa kuwa kweli ni wajenzi wa misingi ya haki, amani na umoja wa kitaifa, daima wakijitahidi kutafuta mafao ya wengi. Mifano bora ya maisha, ni shule tosha kabisa ya utakatifu, unaoweza kuwasaidia wengine kuepuka fursa za dhambi, daima wakijitahidi kujenga uhusiano mwema na Mwenyezi Mungu.

Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Dodoma, ametoa sakramenti ya Kipaimara kwa Wakristo sabini, ambao kwa sasa wanakuwa ni Mabalozi wa Kristo, tayari kumshuhudia kwa ujasiri mkubwa, hata kiasi cha kuyamimina maisha yao. Wameimarishwa na Mapaji ya Roho Mtakatifu, yawawezeshe kuadhimisha vyema Mwaka wa Imani, wakijitahidi pia kuendelea kuiboresha Imani hii, kwa njia ya Neno la Mungu, Maisha ya Kisakramenti pamoja na matendo ya huruma.







All the contents on this site are copyrighted ©.