2012-11-20 14:35:57

Kitabu kuhusu Simulizi za Utoto wa Yesu chazinduliwa!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amezindua kitabu chake kuhusu simulizi za Utoto wa Yesu wa Nazareti na wakati wowote kuanzia sasa, kitabu hiki kitaanza kuuzwa madukani. Kitabu kimekwisha tafsiriwa katika lugha tisa za kimataifa; kati ya hizo kuna: Kiitaliani, Kiingereza, Kifaransa, Kireno, Kihispania, Kijerumani na Kipolandi. Kitabu hiki kimechapishwa katika nchi hamsini na tayari kimekwisha vuka nakala millioni moja.

Taarifa zinabainisha kwamba, katika siku za hivi karibuni, kitabu hiki kitaweza kuchapishwa katika nchi sabini na mbili katika lugha ishirini. Kitabu kimezinduliwa na Kardinali Gianfranco Ravasi, Rais wa Baraza la Kipapa la Utamaduni. Hiki ni kitabu kinachouliza swali la msingi, Je, ni kweli juu ya simulizi zilizoandikwa? Yesu ni nani? NI swali ambalo Yesu mwenyewe aliwahi kuwauliza wafuasi wake kama inavyosimuliwa kwenye Injili ya Marko, lakini ninyi mnasema kuwa mimi ni nani?

Maswali haya msingi yanajibiwa kwa ufasaha kabisa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika kumfahamu Yesu wa Nazareti, kitabu ambacho kina kurasa mia moja na sabini na sita, kimegawanyika katika sura nne, zikiwa na utangulizi mfupi na hitimisho lake. Sura ya kwanza inazungumzia kuhusu ukoo wa Mkombozi kadiri ya Injili ya Mathayo na Luka, wanaotofautiana, lakini wanamwingiza Yesu katika historia na uwepo wake kama mwanzo mpya wa historia ya ulimwengu.

Sura ya pili, inajikita katika tangazo la kuzaliwa kwa Yohane Mbatizaji na Yesu. Baba Mtakatifu anasoma kwa mara nyingine tena mahojiano kati ya Bikira Maria na Malaika Gabrieli, mintarafu Injili ya Luka na kwa njia ya Bikira Maria, mwenyezi Mungu anatengeneza njia mpya ya kuingia duniani, ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika dhambi na mauti, ili kutekeleza dhamana hii, Mwenyezi Mungu anahitaji utii mkamilifu unaojikita katika uhuru wa kutimiza mapenzi ya Mungu. Kwa namna moja, Mwenyezi Mungu anaamua kumtegemea mwanadamu na nguvu yake inategemea jibu la "Ndiyo" ili kuanza historia ya ukombozi.

Sura ya tatu, inaonesha tukio la kuzaliwa kwa Yesu wa Nazareti mjini Bethlehemu; kwa kuwataja wahusika wakuu, wanaomwezesha kuiweka historia hii katika uwanja mpana zaidi wa kimataifa, ili kumkirimia mwanadamu ukombozi kama kielele cha utimilifu wa nyakati. Kila jambo linalosimuliwa hapa lina utajiri mkubwa kuhusu maisha ya Yesu anasema Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita.

Mwana mpendwa wa Mungu anazaliwa katika hali ya umaskini, kielelezo cha mshikamano wa Mungu na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, wanaowakilishwa na wachungaji wanaosikia wimbo wa utukufu wa Mungu ukiimbwa. Baba Mtakatifu anasema, hapa kuna kinzani katika kufasiri maneno yaliyoko kwenye wimbo wa "Utukufu kwa Mungu juu".

Mamajusi na wataalam wa nyota waliiona nyota yake Mashariki, wakaja kumsujudia Mfalme wa Wayahudi pamoja na kukimbilia uhamishoni Misri ni utajiri mkubwa wa simulizi juu ya Utoto wa Yesu wa Nazareti unaopatikana kwenye Sura ya Nne ya Kitabu cha Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita. Mamajusi hawa wanaelezewa kwa kina kwa kuzingatia misingi ya kihistoria na kisayansi, ni watu wanaotafuta kuzima ile kiu ya ndani ya maisha ya mwanadamu.

Baba Mtakatifu anahitimisha kitabu chake kwa kufanya rejea kadiri ya Simulizi za Mwinjili Luka kuhusu Utoto wa Yesu, matukio machache kabisa kabla ya kuanza utume wake hadharani kwa Ubatizo Mtoni Yordani. Tukio la siku tatu, kabla ya kuanza hija ya maadhimisho ya Siku kuu ya Pasaka, pale Yesu alipoamua kubaki nyuma na kuwaacha wazazi wake; Bikira Maria na Yosefu, akaa Hekaluni kwa muda wa siku tatu akijadiliana na Walimu wa sheria. Yesu akazidi kuendelea kukua katika hekima, kimo na neema. Hii ni sehemu inayomwonesha Yesu kuwa ni Mungu kweli na mtu kweli, aliyefikiri na kujifunza katika mtindo wa kibinadamu.

Itakumbukwa kwamba, vitabu viwili vilivyotangulia, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ameandika kuhusu: Maisha ya Yesu Hadharani, tangu alipobatizwa hadi alipogeuka sura na kitabu cha pili ni kuhusu Yesu alipoingia kwa shangwe Yerusalem hadi Ufufuko. Ni vitabu ambavyo vimechapishwa kunako mwaka 2007 na mwaka 2011.







All the contents on this site are copyrighted ©.