2012-11-19 09:07:43

Yesu Kristo ni mwamba wa matumaini thabiti, kamwe hauwezi kuyumba!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili tarehe 18 Novemba 2012, alitafakari kuhusu sehemu ya Injili ya Marko, inayogusia kwa namna ya pekee, mambo ya nyakati za mwisho; yaani: kifo, hukumu, Paradiso na uzima wa milele. Hii pengine ni kati ya sehemu ngumu sana kueleweka kwenye Injili ya Marko, kutokana la ugumu wa yaliyomo na lugha inayotumika.

Ni sehemu ya Injili inayozungumzia mambo yanayozidi ufahamu wa akili ya mwanadamu, jambo linalomfanya Yesu kutumia mifano na maneno kutoka katika Agano la Kale, lakini anakazia kwamba, Yeye mwenyewe ni kiini cha Fumbo hili kutokana na mateso, kifo na ufufuko wake. Injili ya Marko, Jumapili ya thelathini na tatu ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa, anasema Baba Mtakatifu inaonekana kuwa na vitisho, lakini ujumbe unapatikana ile sehemu ya mwisho, watakapomwona Mwana wa Adamu akija mawinguni kwa nguvu nyingi na utukufu.

Yesu mwenyewe anaunganisha historia iliyopita, iliyoko na ile ijayo na kwamba, ni utimilifu wa utabiri uliotolewa na Manabii katika Agano la Kale. Licha vurugu na vitisho vitakavyojitokeza, lakini Yesu anabakia kuwa ni Mwamba thabiti na kamwe hawezi kutikisika! Huu ndio ujumbe wa Injili, Jumapili ya thelathini na tatu ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa, anasema Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita. Neno la Mungu ni kiini cha kazi ya uumbaji na viumbe vyote vinapaswa kuliheshimu Neno la Mungu.

Nguvu ya Uumbaji kutoka katika Neno la Mungu inajikita zaidi kwa Yesu Kristo, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, nguvu inayoongoza mawazo na maneno ya binadamu katika hija ya maisha yake hapa duniani. Yesu anapenda kuwasaidia wafuasi wake kuifahamu ile Siku ya Mwisho, kwa kuondokana na wasi wasi unaojikita katika tarehe na utabiri, anawaonesha njia mwanana wanayopaswa kuitumia ili kufikia maisha ya uzima wa milele. Yesu anasema kwamba, kila kitu kitapita, lakini Neno la Mungu kamwe halitapita na kwamba, kila mtu atahukumiwa kutokana na matendo yake.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anabainisha kwamba, hata nyakati hizi kuna maafa asilia, vita na kinzani mbali mbali. Dunia inahitaji kuwa na Mwamba wa matumaini thabiti ili watu wasitumbukie katika mawazo mepesi mepesi. Anamwomba Bikira Maria awasaidie waamini na watu wenye mapenzi mema, kumpokea Kristo kwa njia ya Neno lake. Anawaalika waamini kuwa waaminifu kwa Mungu na Kanisa, kwa kushiriki kikamilifu Fumbo la Ekaristi Takatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.