2012-11-19 08:30:27

Kanisa Katoliki nchini Nigeria linazidi kukua na kupanuka, matendo makuu ya Mungu!


Askofu mkuu John Olorunfemi Onaiyekan wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria ni kati ya Makardinali wateule watakaosimikwa rasmi Jumamosi ijayo hapa mjini Vatican na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita. Kuteuliwa kwake na Baba Mtakatifu ni ishala ya kukua na kukomaa kwa Kanisa Katoliki nchini Nigeria, licha ya kinzani na changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza katika maisha na utume wa Kanisa.

Tukio la kusimikwa kwake kuwa Kardinali, linatarajiwa kuhudhuriwa na waamini pamoja na watu wenye mapenzi mema zaidi ya mia mbili kutoka Nigeria, kadiri ya taarifa iliyotolewa na Padre Patrick Tor Alumuku, mkurugenzi wa Idara ya Mawasiliano, Jimbo kuu la Abuja, Nigeria.

Tangu kuteuliwa kwake, Kardinali mteule Onaiyekan ameendelea kupokea ujumbe wa pongezi na matashi mema kutoka kwa viongozi wakuu wan chi na Kanisa ndani na nje ya Nigeria. Waamini wanaendelea kumshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, hata kwa kumteua Monsinyo Fortunatus Nwachukwu, kuwa Askofu mkuu na Balozi wa Vatican nchini Nicaragua. Zote hizi ni dalili za kukua na kukomaa kwa Kanisa Katoliki nchini Nigeria, kiasi kwamba, linaweza kuchangia katika maisha na utume wa Kanisa la kiulimwengu. Kuna idadi kubwa ya waamini nchini Nigeria na kwamba, miito inazidi kuongezeka siku hadi siku.

Kanisa nchini Nigeria ni mhimili mkuu wa maendeleo ya watu: kiroho na kimwili; dhamana inayojionesha kwa namna ya pekee kabisa katika utoaji wa huduma kwenye sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu ya wananchi wa Nigeria. Kwa sasa Kanisa linaendelea kuwekeza katika maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari, ili kuweza kufikisha ujumbe wa imani, matumaini na mapendo kwa watu wengi zaidi, ikilinganishwa na hali ya sasa.








All the contents on this site are copyrighted ©.