2012-11-19 07:55:31

Askofu mkuu Guido Pozzo awekwa wakfu: kielelezo cha huduma ya upendo wa Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa wahitaji zaidi


Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican, mwishoni mwa juma, amemweka wakfu Monsinyo Guido Pozzo, aliyeteuliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi wa kumi na sita kuwa Mhudumu mkuu wa Sadaka ya Papa, kuwa Askofu mkuu. RealAudioMP3

Ibada hii imefanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Lorenzo in Damaso. Ni mtu ambaye Baba Mtakatifu anamfahamu fika, kwani walikwishawahi kufanya kazi kwa pamoja katika Baraza la Mafundisho Sadikifu ya Kanisa na sasa kwa kuwekwa wakfu anakuwa ni sehemu ya Familia ya Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Katika mahubiri yake, Kardinali Bertone anasema kwamba, furaha ya kweli inapatikana kwa kujitoa bila ya kujibakiza katika utoaji wa huduma makini, hasa pale anapoadhimisha na kuwagawia waamini Mafumbo ya Kanisa; hapa inakuwa kweli ni chemchemi ya furaha inayobubujika kutoka katika Imani kwa Kristo na Kanisa lake. Furaha hii ioneshe moyo wa mshikamano, utambulisho wa kuwa Mkristo na Imani ya kweli. Ni mwaliko wa kuwagawia wengine, imani, matumaini na mapendo.

Kwa kuwekwa kwake wakfu kuwa Askofu mkuu, jina lake linaandkiwa katika kitabu cha waandamizi wa mitume, wale ambao kwa njia ya Roho Mtakatifu wanaendeleza Kanisa la Mungu, kama wachungaji na walimu wa Kanisa.

Kwa namna ya pekee, Kardinali Bertone anawaalika waamini kuwa na imani na matumaini kwa Kristo na kamwe wasikubali kuelemewa na vitisho vinavyosimuliwa katika Liturujia ya Neno la Mungu, Jumapili ya thelathini na tatu ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa. Watambue kwamba, Kristo atakuja tena kuwahukumu wazima na wafu na wala ufalme wake hautakuwa na mwisho, changamoto kwa wafuasi wa Kristo kumwilisha ndani mwao Injili ya Upendo. RealAudioMP3

Mama Kanisa anatumwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa kuwashirikisha wote ule upendo unaibubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu; upendo unaobubujika kutoka katika Sakramenti za Kanisa na huduma bora kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili waonje joto la imani inayotolewa ushuhuda wa kweli katika mshikamano wa upendo.Waamini wanachangamotishwa kutolea ushuhuda wa imani yao kwa ari na moyo mkuu. Huu ndio utume ambao Askofu mkuu Guido Pozzo anaalikwa kuutekeleza kwa niaba ya huduma ya upendo inayotolewa na Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Ni huduma ya upendo na mshikamano inayojikita katika maisha ya kawaida kabisa na wakati mwingine katika hali ya ukimya kama kielelezo cha udugu na mshikamano wa Kikristo, changamoto endelevu inayotolewa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa maskini, wahitaji na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Huduma ya upendo ni utume wa kila mwamini anasema Kardinali Bertone, lakini ni wajibu fungamanishi kwa viongozi wa Kanisa waliyopewa dhamana ya kuwaongoza, kuwafundisha na kuwatakatifuza watu wa Mungu waliokabidhiwa kwao. Ni wajibu wao kutekeleza dhamana hii mintarafu dira na mwongozo wa Yesu Kristo mchungaji mwema.

Huduma ya upendo inaunganisha utambulisho wa kitaalimungu na maisha ya kiroho yanayojionesha kwa namna ya pekee kwa Askofu anapotekeleza utume wake katika shughuli za kichungaji. Ni mwaliko wa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake, kwa njia hii, Kristo anaendelea kumhudumia mwanadamu.

Hii ndiyo changamoto endelevu atakayokabiliana nayo Askofu mkuu Guido Pozzo wakati wa utekelezaji wa dhamana na utume wake kwa Kanisa. Umefika wakati wa kudhihirisha yale majiundo makini aliyoyapata katika hatua mbali mbali za maisha yake kama Padre na sasa kama Askofu; ni muda wa kuonesha upendo mkamilifu kwa Kristo, Kanisa na Khalifa wa Mtakatifu Petro na kuendelea kushuhudia utajiri wa huduma aliyokuwa anaitoa kwa miaka mingi hapa Vatican, katika nyadhifa mbali mbali alizokabidhiwa na Mama Kanisa.









All the contents on this site are copyrighted ©.