2012-11-17 10:10:54

Wahudumu wa sekta ya afya tangazeni Injili ya Upendo, Uhai na Matumaini kwa kuwa waaminifu, makini na wenye huruma!


Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi katika sekta ya afya, Jumamosi, tarehe 17 Novemba 2012 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro Mjini Vatican kwa ajili ya washiriki wa Kongamano la Madaktari Wakatoliki kutoka Ulaya uliokwenda sanjari na Mkutano wa ishirini na saba wa afya kimataifa ulioandaliwa na Baraza lake. RealAudioMP3

Katika mahubiri yake, Askofu mkuu Zimowski amewaalika wafanyakazi katika sekta ya afya kuendelea kuwa waaminifu katika maisha na utume wao kwanza kabisa kwa Kristo na Kanisa; kwa wagonjwa na wote wanaoteseka wakitambua kwamba, wao kimsingi wanaalikwa kuhudumia Injili ya Uhai, kwani maisha ya mwanadamu ni matakatifu kwa sababu yanapata chimbuko lake kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Anawataka wawe wahudumu makini, daima wakiendelea kukesha na kusoma alama za nyakati mintarafu Mafundisho ya Kanisa. Watoe huduma kwa wagonjwa huku wakisukumwa na huruma kutoka kwa Mwenyezi Mungu, daima wakijitahidi kutenda mema na wala wasikatishwe tamaa katika huduma na maisha yao ya Kikristo.

Mambo makuu matatu wanapaswa kuyazingatia nayo ni kukesha kwani hawajui siku wala saa atakapokuja Mwana wa Mtu. Hiki kiwe ni kipindi cha kutekeleza mapenzi ya Mungu katika hija ya maisha yao hapa duniani; ni mwaliko wa kuwasha taa ya imani inayomwilishwa kwa njia ya upendo wa dhati; changamoto iliyofanyiwa kazi na watakatifu wengi ndani ya Kanisa.

Anawaalika waamini kwa namna ya pekee, kumtafuta, kumpenda na kumhudumia Kristo kwa njia ya ndugu zake walio wadogo zaidi, wanaoelemewa na magonjwa, uzee, upweke na wakati mwingine wanabaguliwa kutokana na hali yao ya maisha. Wote hawa waonjeshwe Injili ya Upendo.

Wafanyakazi wa sekta ya afya, kimsingi ni watangazaji wa Injili ya Uhai ambayo wanapaswa kuwaonjesha jirani zao kwa njia ya huduma makini, ukweli na ushuhuda wa maisha yao, hasa katika ulimwengu mamboleo ambamo watu wengi wanakabiliwa na ukavu wa maisha ya kiroho kutokana na kuelemewa na malimwengu; wote hawa wanahitaji waamini wanaojifunga kibwebwe ili kushuhudia imani yao sanjari na kuyatakatifuza malimwengu.

Ni changamoto ya kusimama kidete dhidi ya Utamaduni wa kifo, kwa kutangaza kwa nguvu na ari kuu zaidi Utamaduni wa uhai, kwa kutambua na kuenzi utambulisho wao unaopata chimbuko lake katika Ukristo.

Injili ya Kristo iwe ni dira na mwongozo katika utekelezaji wa majukumu la taaluma yao, kwani Injili ya Matumaini kamwe haiwezi kumdanganya mtu! Utume huu wanapaswa kuutekeleza kwa ujasiri mkubwa Barani Ulaya kwa kutangaza Injili ya Matumaini kwa watu wanaokata tamaa, lakini zaidi, kwa kuwahudumia wagonjwa na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Waimarishe Imani yao kwa njia ya ushiriki wao katika Fumbo la Ekaristi Takatifu, wanamo tangaza: mateso, kifo na ufufuko wa Kristo, kiini cha Imani ya Kanisa.

Utangazaji wa Injili ya Matumaini ujioneshe hasa katika maeneo ya kazi kwa kulinda na kutetea: maisha, utu na heshima ya mwanadamu; umoja na mshikamano kati ya watu, kwani wote hawa wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu: wawe ni vyombo vya upatanisho barani Ulaya, vinavyomwelekea Yesu Kristo mkombozi wa ulimwengu.







All the contents on this site are copyrighted ©.