2012-11-17 08:31:11

Kilele cha utamadunisho ni kushiriki katika utukufu wa Kristo!


Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican, Padre Nikodemo Mayala katika makala haya amefafanua vyema dhana nzima ya utamadunisho na kwamba, kilele cha utamadunisho ni kutaka kushiriki utukufu wa Kristo, kwa kupata maisha ya uzima wa milele. Ninakusihi uendelee kujichotea utajiri wa makala hii, ukiweza mshirikishe na jirani yako pia, kwani utamadunisho ni dhamana endelevu katika hija ya maisha ya waamini. RealAudioMP3
Tamaduni zinapokutana hutokea nini?
Mkutano, mawasiliano na mgusano wa tamaduni. Utamaduni wa kigeni kukutana na utamaduni wa wakazi. Hatua hii muhimu hukanganya, maana mgeni huja na chake, na mwenyeji analinda chake. Kila mmoja anathamini chake. Chake ni bora kuliko! Mawasiliano ya awali ni mgongano na msuguano. Kukosa kuelewana, kupambana. Jitihada ya wazi ni kujihami kwa kila namna. Ni hatua ya msingi kutafititi kutofautisha tamaduni mbili katika msuguano. Wangu bora, wako bora!

Tutambue tamaduni zote si kamilifu. Hivi mwingiliano ni wa lazima ili kutajirishana. Itakumbukwa kuwa alipofika mkoloni na mlowezi, aliukoloni utamaduni, akaulowa utamaduni wa watu akapandikiza wa kikoloni. Fahari ni kulonga kiingereza, kifaransa na kireno. Huu ndo uliitwa utamadunisho, ustaraabisho. Aidha, Kanisa lilipopandikizwa, Kilatini ilikuwa kama lugha ya Mungu. Si lugha ya mawasiliano kukutana na tamaduni za watu. Lakini Mungu katika nyakati zetu “amesema na sisi katika Mwana” (Ebr.1:2).

Ikumbukwe kwamba, kwa sasa wale wote wanaopania kuwa Mapadre, wanapaswa kuifahamu lugha ya Kilatini, kama anavyokazia Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kumbe lugha ya Kilatini kwa Kanisa bado ina umuhimu wa pekee.

Mlishizo. Hatua hii ni mithili ya kulishiza chakula baada ya mmeng’enyo , kufanya mwenyeji; staarabika, staarabisha, similisha chukua, pata (maarifa, fikira,n.k.). Tutakumbuka mlishizo, usimilishaji kuwa ilikuwa sera ya Wareno na Wafaransa katika harakati zao kuwageuza wenyeji wafanane kama wao. Mlishizo Injili ni ustaarabishaji wa wakazi kiinjili, kuwafanya wafanane na Kristo, si tena na mreno wala mfaransa.

Mapinduzi ya kitamaduni: Mageuzoumbile, mabadilikoumbile. Hatua hii muhimu ya mabadiliko ni ya makuzi. Tamaduni zinatajirishana, zinatakasana, na kila upande waafiki uongofu. Mapokezi ya mageuzo na mbadiliko yanaunda utamaduni fungamanifu.

Twaweza kufananisha mabadiliko umbile ya utamaduni na tukio la mng’aro wa Bwana wetu Yesu Kristo kule mlimani kuwa ndo kilele cha utamadunisho.

Kutamadunisha twamanisha nini? Utamadunisho kwetu ni wongofu. Watu wamwongekee Mungu. Utamadunisho ni kuruhusu Neno kukua na kukomaa kwa kutumia virutubisho mahalia. Kwa maneno mengine utamadunisho wamanisha kuwa Ukristo waweza kuota mizizi utakapotwaa mwili katika mifumo ya tamaduni. “Maana ilimpendeza Roho Mtakatifu na sisi, tusiwatwike mzigo ila hayo yaliyo ya lazima.”(Mdo.15:28). Utamadunisho ni kukiri, kutambua utambulisho na tofauti. Mambo ya msingi ni wongofu na ukamilifu. Mwanadamu atafute kumwongea Mungu ili apate ukamilifu katika Mungu.

Utamadunisho wajumuisha: mawasiliano, tafsiri (toa mawazo kutoka katika lugha moja kwenda nyingine bila ya kubadilisha maana; eleza maana ya maneno kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine; Je, Mawazo yaliyotolewa kutoka lugha moja kwenda hadi nyingine; maelezo kutoka lugha moja hadi nyingine), ukalimani/ufasiri: eleleza maana ya maneno kutoka lugha moja hadi nyingine, fafanua, uhariri: tengeneza maandishi kwa kuyasahihisha, kuyarekebisha na kuyapanga kwa ajili ya kuchapa katika gazeti au kitabu, tengeneza. Tahariri, maelezo, maoni au fikira zinazotolewa na mhariri juu ya jambo fulani katika gazeti, jarida au kitabu.

Mayala, Nikodemo
Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.