Baba Mtakatifu Benedikto XVI kuzindua kitabu chake kuhusu Simulizi za Utoto wa Yesu
Kitabu cha Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kuhusu Simulizi za Utoto wa Yesu,
kinatarajiwa kuzinduliwa rasmi hapo tarehe 20 Novemba 2012 hapa mjini Roma. Kati ya
wahamasishaji wakuu ni pamoja na Kardinali Gianfranco Ravasi, Rais wa Baraza la Kipapa
la Utamaduni, Maria Clara Bingemer, Jaalim wa taalimungu kutoka Chuo Kikuu cha Kipapa
cha Rio de Janeiro.
Wengine ni: Padre Giuseppe Costa, Mkurugenzi wa Idara ya
Uchapaji ya Vatican pamoja na Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican ambaye
ataratibu shughuli zote za uzinduzi wa kitabu hiki kinachotarajiwa kuwa ni msaada
mkubwa kwa waamini wakati wa Kipindi cha Majilio na hasa zaidi wakati huu Mama Kanisa
anapoendelea kuadhimisha Mwaka wa Imani, changamoto kwa waamini kuifahamu kwa undani
zaidi imani yao ili hatimaye, waweze kuitolea ushuhuda makini.