Majadiliano ya kiekumene ni sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya unaodai wongofu
wa ndani na ushuhuda amini miongoni mwa Wafuasi wa Kristo
Mama Kanisa katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, anaendelea kukazia umuhimu wa majadiliano
ya kiekumene kama mtindo wa Uinjilishaji mpya. Huu ndio mwendelezo ulioneshwa kwa
namna ya pekee na Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji mpya iliyohitimishwa
hivi karibuni hapa mjini Vatican. Ndiyo mada ambayo pia imeongoza mkutano wa Baraza
la Kipapa la uhamasishaji umoja wa Wakristo, uliohitimishwa kwa kukutana na Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita mjini Vatican, siku ya Alhamisi, tarehe 15 Novemba, 2012.
Mwaka
wa Imani unakwenda sanjari na kumbu kumbu ya Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya
Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, ambamo Mababa wa Mtaguso walikazia kwa namna ya pekee,
dhamana ya Uinjilishaji sanjari na jitihada za kujenga umoja miongoni mwa Wakristo,
ili wote wawe wamoja kadiri ya utashi wa Kristo, kwani utengano ni kashfa kubwa kwa
Wakristo duniani na una athari kubwa katika mchakato wa Uinjilishaji.
Wakristo
hawana budi kuongeza juhudi za kujipatanisha kama alivyotaka Kristo mwenyewe katika
ile sala ya kikuhani, ambayo anakazia umoja na mshikamano miongoni mwa wafuasi wake,
ili dunia iweze kuamini kwamba, ametumwa na Baba yake wa mbinguni. Kuna uhusiano mkubwa
kati ya Uinjilishaji na ushuhuda unaofumbatwa katika Umoja wa Wakristo.
Hayo
yamesemwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati alipokutana na wajumbe
wa Baraza la Kipapa la uhamasishaji wa Umoja wa Wakristo, anayeendelea kuhimiza umoja
na mshikamano miongoni mwa wafuasi wa Kristo, kama kielelezo makini cha kutangaza
Imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Watu wana kiu ya maisha ya kiroho, wanakabiliana
na umaskini wa kiroho, kiasi kwamba, wanashindwa kutambua uwepo wa Mungu katika maisha
yao.
Hii ni changamoto kwa wakristo wote kuzima kiu hii ya maisha ya kiroho,
kwa kuonesha njia inayojikita katika ushuhuda wa imani kwa Mungu aliye hai; anayefahamu
na kupenda, ambaye yuko karibu na waja wake; Mungu anayesubiri kwa uvumilivu mkubwa
jibu la upendo kutoka kwa mwanadamu katika hija ya maisha yake ya kila siku. Huu ni
mwaliko anasema Baba Mtakatifu kwa Wakristo wote kuchangamkia utangazaji wa Injili
ya Kristo kwa watu wa ulimwengu mamboleo.
Ni ushuhuda unaomwonesha Mungu ambaye
amejifanya jirani kwa binadamu kwa njia ya Yesu Kristo, dhamana ya kuchuchumilia umoja
na mshikamano miongoni mwa wafuasi wa Kristo, wanaotambua kwamba, wanaunganishwa pamoja
kwa njia ya Imani kwa Mungu, Baba na Muumba, aliyejifunua kwa njia ya Yesu Kristo,
akawakirimia waja wake Roho Mtakatifu anayetakatifuza na kujenga. Hii ndiyo imani
ya Ubatizo ambayo waamini wameipokea katika matumaini na mapendo, wanayoweza kuiungama
kwa pamoja.
Baba Mtakatifu anakazia umuhimu wa kuendeleza majadiliano ya kitaalimungu,
dhamana ambayo Kanisa Katoliki linaipatia kipaumbele cha pekee, ingawa bado kuna njia
ndefu ili kuweza kufikia umoja kamili. Hija ya majadiliano iwawezeshe waamini kushirikishana
utajiri na mang'amuzi ya maisha ya kiroho na kweli za kitaalimungu, ili kuhamasisha
ushuhuda wa imani.
Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, wakristo wanapaswa kujitoa
kimaso maso katika kudumisha umoja miongoni mwao, lakini watambue kwamba, hizi si
juhudi zao binafsi, bali ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na inaweza kupatikana
kwa njia ya Yesu mwenyewe kwani Kanisa ni lake. Kumbe, Uinjilishaji mpya ni mwaliko
wa kutembea pamoja kwa kurekebisha kasoro na misigano ili umoja wa kweli uweze kuonekana.
Ni
matumaini ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwamba, katika maadhimisho
ya Mwaka wa Imani, utasaidia pia kukuza na kukoleza majadiliano ya kiekumene, umoja
na imani kama njia ya ushuhuda amini kwa wale wasiomwamini Yesu Kristo Mkombozi wa
ulimwengu au wale ambao wamemezwa zaidi na malimwengu licha ya kubahatika kusikia
Habari Njema ya Wokovu ikitangazwa maishani mwao. Majadiliano ya kiekumene kwanza
kabisa ni kutambua kazi ya Mungu, kwa uvumilivu na unyenyekevu wa hali ya juu kwa
kupania kutekeleza mapenzi ya Mungu.
Majadiliano ya kiekumene ni sehemu ya
mchakato wa Uinjilishaji Mpya unaodai wongofu wa ndani na utashi wa kumfuasa Kristo
pamoja na kutekeleza mapenzi ya Mungu.