2012-11-15 08:07:58

Changamoto zinazojitokeza katika kuendesha taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu Barani Afrika


Monsinyo Pius Rutechura Makamu mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Afrika Mashariki na Kati, CUEA, katika mahojiano na Radio Vatican anabainisha changamoto kadhaa wanazokabiliana nazo katika harakati za kuendesha taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu vya Kikatoliki Afrika Mashariki, lakini kwa namna ya pekee, CUEA. RealAudioMP3

Anasema, wanapaswa kuwa macho na makini katika kuandaa na kuendesha programu za masomo zinazokidhi mahitaji ya elimu katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia; programu ambazo zinapania kumwendeleza mtu mzima: kiroho na kimwili.

Kutokana na myumbo wa uchumi kimataifa, taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu havina budi kuhakikisha kwamba, vinatafuta vyanzo mbali mbali vya fedha nje ya karo inayotolewa na wanafunzi, ili kuweza kufanya maboresho zaidi katika mfumo wa elimu inayotolewa vyuoni hapo. Juhudi hizi ni sehemu ya mchakato wa kutaka kujitegemea kwa kiasi kikubwa.

Katika ulimwengu mamboleo, hatoshi kuwa na cheti, bali Jamii inaangalia zaidi ubora na viwango vya elimu inayotolewa chuoni hapo, ili kukabiliana na ushindani unaojitokeza katika taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu sehemu mbali mbali za dunia. Ubora lazima ukidhi viwango vya kitaifa na kimataifa sanjari na kujenga ushirikiano wa dhati na vyuo vingine.

Monsinyo Rutechura anasema kwamba, kuna haja ya kubadilisha mtindo wa uongozi kwa kujikita zaidi katika ushirikiano na umoja; utunzaji bora wa kumbu kumbu pamoja na viongozi wenyewe kujiamini kwamba, wanaweza kutekeleza dhamana waliyokabidhiwa na Kanisa pamoja na Jamii katika ujumla wake. Yote haya ni mambo msingi yanayopaswa kuzingatiwa ili kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazoendelea kuibuka siku hadi siku katika sekta ya elimu ya juu.







All the contents on this site are copyrighted ©.