Wainjilishaji, jiinjilisheni kwanza, ili muweze kuwainjilisha wengine kwa umakini
mkubwa zaidi!
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na
sita, yawe ni fursa muhimu sana kwa waamini, lakini zaidi kwa viongozi wa Kanisa kuweza
kuikimbilia huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho, ili Sakramenti
hii iweze kuwa ni dira na mwongozo wa maisha kwa viongozi wenyewe na wale ambao Mama
Kanisa amewapatia dhamana ya kuwaongoza. Lengo kuu ni kuchuchumilia utakatifu wa maisha,
kwa njia ya kuyatakatifuza malimwengu kwa chachu ya Sakramenti za Kanisa.
Ni
maneno ya Kardinali Timothy Dolan, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani, alipokuwa
anafungua mkutano wa Maaskofu mapema juma hili. Maaskofu wanatambua taabu na mahangaiko
ya watu wao yaliyojitokeza hivi karibuni kutokana na tufani, changamoto za Uinjilishaji
Mpya kama zilivyobainishwa na Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya,
Fursa mbali mbali za kukuza, kuimarisha na kutolea ushuhuda imani pamoja na umuhimu
wa kuendeleza majadiliano ya kidini, kiekumene na kitamaduni.
Kanisa linakabiliana
na changamoto pevu ya kuendelea kusimama kidete kwa kupaaza sauti yao ya kinabii,
katika kulinda na kutetea Injili ya Uhai, tunu msingi za maisha ya ndoa na familia,
utu na heshima ya mwanadamu, bila kuwasahau wale ambao bado wanaogelea katika dimbwi
la umaskini, ujinga na njaa. Bado kuna kundi kubwa la wakimbizi na wahamiaji wanaopaswa
kulindwa na kutetewa haki zao msingi na kwamba, Kanisa lina wajibu wa kusikiliza kilio
cha watu wanaoteseka na kudhulumiwa sehemu mbali mbali za dunia sanjari na kuimarisha
uhuru wa binadamu.
Kardinali Dolan anawakumbusha Maaskofu kwamba, wao kama
viongozi wa Kanisa, wanapaswa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kumfuasa Kristo,
wakitambua kwamba, kwao Yesu ni: Mwana wa Mungu, Mkombozi wa dunia, rafiki na mwenza
katika hija ya maisha, kwani alikwisha kusema kwamba, Yeye ni njia, ukweli na uzima,
mwaliko kwa wafuasi wake kutafuta kwanza ufalme wa Mungu na mengine watapewa kwa ziada.
Yesu
anapaswa kuwa ni kiongozi wao katika mchakato wa majadiliano ya: kitamaduni, kidini
na kiekumene, daima wakijitahidi kutubu na kuongoka, kama changamoto endelevu iliyotolewa
na Mababa wa Sinodi juu ya Uinjilishaji Mpya, kwani Uinjilishaji mpya unawachangamotisha
kujiinjilisha kabla ya kuwainjilisha wengine, ili kweli Injili ya Kristo iweze kupata
nafasi katika maisha ya watu wa ulimwengu mamboleo.
Mihimili ya Uinjilishaji
haitaweza kuvuna matunda mengi anakumbusha Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita,
ikiwa kama wao wenyewe hawatachukua hatua madhubuti za Kujiinjilisha kwanza. Maaskofu
katika maisha na utume wao, lazima wachuchumilie toba na wongofu wa ndani, ili kweli
waweze kuwa ni vyombo vinavyohamasisha upya wa maisha yanayopata chimbuko lake kutoka
kwa Kristo. Ili changamoto hii iweze kufanikiwa, kuna haja ya kufufua na kuimarisha
moyo na ari ya kutaka kupokea Sakramenti ya Upatanisho mara kwa mara.
Kardinali
Dolan anasema, kwa hakika Sakramenti ya Upatanisho ni kwa ajili ya wainjilishaji,
ili waweze kujiinjilisha na hatimaye, kuwainjilisha wengine, ili waweze kukutana na
Yesu Kristo Mkombozi wa dunia, anayewaonjesha huruma na upendo wake; Yesu anayewaalika
kutubu na kuongoka, ili waweze kuyatakatifuza malimwengu kwa chachu ya Injili.
Sakramenti
ya Upatanisho ni changamoto endelevu iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili
wa Vatican, katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, waamini wajitahidi kuipatia kipaumbele
cha pekee, kwa kutambua umuhimu wake katika maisha na utume wa Kanisa. Kwa hakika
Sakramenti ya Upatanisho ni Sakramenti ya Uinjilishaji Mpya.