2012-11-13 07:28:45

Vyuo vikuu vya Kikatoliki vinavyojipanga kucharuka katika maboresho ya viwango vya elimu sehemu mbali mbali za dunia!


Monsinyo Pius Rutechura, Makamu mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Afrika Mashariki na Kati, CUEA ni kati ya wajumbe kutoka vyuo vikuu vya kikatoliki walioshiriki katika mkutano wa wakuu wa vyuo hivi kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Mkutano wa wakuu wa vyuo vya kikatoliki uliwakutanisha na Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki ili kubainisha mwelekeo wa vyuo vikuu vya kikatoliki katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. RealAudioMP3

Wamepata nafasi ya kuweza kufafanua kwa kina na mapana utambulisho wa vyuo vikuu vya kikatoliki, taswira, malengo na utume wake ndani ya Jamii husika. Wamegusia ubora na viwango vinavyotakiwa, kwa kuzingatia na kuheshimu: maadili, kanuni, urithi na Mapokeoa ya utamaduni wa utoaji wa elimu kutoka katika vyuo vya kikatoliki sehemu mbali mbali za dunia.

Imekuwa ni nafasi ya pekee anasema Monsinyo Rutechura kwa wajumbe kupembua jinsi ambavyo vyuo hivi vinaendelea kutoa elimu ya juu, usimamizi na maandalizi ya wale wenye dhamana ya maboresho ya viwango na ubora wa elimu ya juu. Kila Chuo kilipata nafasi ya kuangalia programu zake, vianzio vya fedha katika jitihada nzima za kutaka kujitegemea, maboresho katika mfumo wa uongozi, ili uweze kukidhi mahitaji na matarajio ya watu wa Karne ya ishirini na moja.

Wajumbe kwa pamoja, wamekazia umuhimu wa kudumisha na kuendeleza mshikamano wa kimataifa ili kusonga mbele katika harakati za kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la ujinga, umaskini na magonjwa.







All the contents on this site are copyrighted ©.