2012-11-13 09:11:39

Papa atangaza nia binafsi ya kuanzisha Taasisi Mpya ya Lugha ya Kilatini


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa utashi wake mwenyewe, ameanzisha Taasisi ya Lugha ya Kilatini, kwa kutambua umuhimu wake ndani ya Kanisa Katoliki, tangu wakati ule wa Pentekoste, waamini wa Kanisa la Mwanzo walipokuwa wanazungumza lugha mbali mbali, lakini wakaelewana.

Tangu awali, anasema Baba Mtakatifu katika Waraka unaonesha nia yake ya kuanzisha Taasisi ya Lugha ya Kilatini kwamba, lugha ya Kigiriki na Kilatini zimekuwa zikitumiwa na Mama Kanisa katika mawasiliano. Baada ya kutoweka kwa Himaya ya Kirumi, Kanisa Katoliki likaendelea si tu kutumia lugha ya Kilatini, bali likawa ni msimamizi na mhamasishaji wake mkuu sehemu mbali mbali za dunia, kiasi cha kutumika katika taalimungu. liturujia, majiundo na urithishaji wa maarifa.

Hata leo hii anasema Baba Mtakatifu, Lugha ya Kilatini ina umuhimu wake kwa watu na tamaduni mbali mbali, kwani ni chemchemi ambayo watu wasomi na wanazuoni wanakwenda kuzima kiu yao ya ufahamu na bado inaendelea kutumika katika masomo ya Falsafa na Taalimungu kwa ajili ya Mapadre wa baadaye. Wasomi wengi wanaendelea kukuza ari ya kutaka kujichotea utajiri wa unaofumbatwa katika lugha ya Kilatini katika masuala ya sayansi na teknolojia.

Huu ndio mwelekeo mpya unaojionesha katika ulimwengu mamboleo kwa kuwahusisha vijana wengi zaidi kutoka katika tamaduni mbali mbali duniani. Ndiyo maana anasema Baba Mtakatifu kuna haja ya kuwachangamotisha watu wengi zaidi kupenda kujifunza na kuifahamu lugha ya Kilatini katika mazingira ya Kanisa na katika tamaduni mbali mbali, kwa kuwa na mbinu makini za ufundishaji ili kuunganisha nguvu na taasisi nyingine zinazojikita katika ufundishaji wa lugha ya Kilatini, bila kuwasahau wasomi wanaoitumia lugha hii.

Lengo ni kuonesha kipaumbele cha pekee katika utajiri unaofumbatwa kwenye utamaduni wa lugha ya Kilatini. Baba Mtakatifu anaendelea kusema kwamba, anafuata nyayo za watangulizi wake ili kufanikisha lengo hili, ndiyo maana kwa utashi wake mwenyewe ameamua kuanzisha Taasisi Mpya ya Lugha ya Kilatini, itakayokuwa chini ya usimamizi wa Baraza la Kipapa la Utamaduni. Itaongozwa na Rais pamoja na Katibu mkuu watakaoteuliwa na Baba Mtakatifu mwenyewe pamoja na Baraza la Elimu.








All the contents on this site are copyrighted ©.