2012-11-12 15:07:50

Wazee ni tunu muhimu katika Jamii; wanapaswa kupokelewa, kuheshimiwa; wanateseka katika ukiwa, wanapotengwa na kuelemewa na upweke


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumatatu tarehe 12 Novemba 2012 ametembelea nyumba ya wazee inayohudumiwa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio kama sehemu ya maadhimisho ya Mwaka wa Wazee Barani Ulaya na mshikamano kati ya kizazi na kizazi. Baba Mtakatifu ametumia fursa hii kuishukuru Jumuiya ya Mtakatifu Egidio pamoja na Wasamaria wema wanaoendelea kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kuwahudumia wazee wanaotunzwa katika Jumuiya hiyo.

Baba Mtakatifu anasema, anawatembele kwa nafasi yake kama Askofu wa Roma, lakini zaidi kama mzee mwenzao, anayefahamu fika matatizo na changamoto zinazojitokeza katika umri kama huu na hasa zaidi wakati huu kutokana na myumbo wa uchumi kimataifa, hali inayoweza kuwajengea kishawishi cha kutamani yale yaliyopita wakati walipokuwa bado vijana, wakiwa na nguvu na mipango lukuki kwa siku za usoni. Hali hii inaweza pia kuwajengea simanzi na huzuni. Licha ya matatizo na changamoto wanazokabiliana nazo wazee sehemu mbali mbali za dunia, lakini, anapenda kuwahakikishia kwamba, kwa hakika inapendeza kuwa mzee!

Kila umri una baraka na utajiri wake na kamwe watu wasigubikwe na simanzi, kwani wamebahatika kupata maisha marefu na kwamba, kuishi katika umri wao huo ni jambo jema kabisa, licha ya vizingiti na vikwazo vinavyoweza kujitokeza, lakini wanapaswa kutambua kwamba, kweli wanapendwa na Mwenyezi Mungu, hivyo, hakuna sababu ya kujawa na majonzi.

Katika Biblia anasema Baba Mtakatifu, maisha marefu yalihesabiwa kuwa ni baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu, inayopaswa kupokelewa kama zawadi, kwa kuthaminiwa na kutunzwa. Wazee ni tunu muhimu sana katika Jamii na wala si watu wanaopaswa kubezwa. Wazee wanateseka pale wanapotengwa, wanapoishi mbali na nyumba zao na zaidi sana wanapojikuta wakielemewa na upweke.

Baba Mtakatifu anashauri kuanza jitihada zitakazoziwezesha Familia kuweza kuwatunza wazee nyumbani mwao, ili waweze kujichotea hekima, ujuzi, maarifa na mang'amuzi waliojitwalia katika hija ya maisha yao. Ubora wa maisha ndani ya Jamii husika unapimwa na jinsi ambavyo Jamii hiyo inawatunza na kuwajali wazee wake, kwani hawa ni watu ambao wana hekima na hivyo utajiri wanaoubeba ndani mwao, hauna budi kuthaminiwa. Jamii inayotoa nafasi kwa wazee, hiyo itambue kwamba, inapokea zawadi ya maisha.

Baba Mtakatifu anaishukuru kwa namna ya pekee, Jumuiya ya Mtakatifu Egidio ambayo imekuwa mstari wa mbele kuwahudumia wazee na watu mbali mbali wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili kutambua kwamba, Kanisa ni kielelezo cha mshikamano na watu wa vizazi vyote unaofumbatwa katika upendo. Thamani ya maisha na utu wa mwanadamu havipungui kwa uzee, kwani kila mtu katika umri mbali mbali amenuiwa na kupendwa na Mwenyezi Mungu, kumbe, ana maana na umuhimu wake.

Baba Mtakatifu anasema katika maadhimisho ya Mwaka wa Wazee anapenda kusisitiza kwamba, wazee ni tunu muhimu sana katika maisha ya Jamii, hasa zaidi kwa vijana, kwani wazee ni sawa na kitabu ambacho kiko wazi, na vijana wa kizazi kipya wanaweza kupata miongozo ya maisha. Katika uzee, mtu atatendewa hata kinyume cha utashi wake, kiasi cha kutolea ushuhuda wa maisha yake, lakini wamshukuru Mungu pia kwa huduma inayotolewa na jirani zao, kwani kila mtu anamtegemea mwingine, ili kujenga na kuimarisha mfumo wa Familia inayojengeka katika upendo.

Baba Mtakatifu anawaambia wazee wenzake kwamba, kuna wakati wanajisikia kwamba, muda wao hauna maana tena, umesheheni utupu na matatizo, hakuna watu wa kukutana nao wala mambo wanayopaswa kutekeleza, haya yote yasiwakatishe tamaa; hata pale wanapokabiliana na magonjwa na mateso, daima wakumbuke kwamba, maisha ni zawadi ili kujenga na kuimarisha uhusiano na Mwenyezi Mungu. Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili hadi leo hii ni mfano na kielelezo cha kuigwa.

Baba Mtakatifu anawahimiza wazee kuendelea kusali kwa imani bila kuchoka, kuliombea Kanisa na viongozi wake, mahitaji ya dunia na maskini, ili haki na amani viweze kutawala duniani. Sala ya wazee inaweza kuilinda dunia. Baba Mtakatifu amewakabidhi wazee hao jukumu la kuliombea Kanisa na amani duniani. Watambue kwamba, anawapenda na kuwajali, kama wanavyopendwa pia na Mwenyezi Mungu, wasikatishwe tamaa na ubinafsi unaojitokeza ulimwenguni kwa kujali zaidi tija.







All the contents on this site are copyrighted ©.