2012-11-12 07:25:41

Kazi ni wajibu na utimilifu wa utu na heshima ya binadamu, ijikite daima kutafuta mafao ya familia


Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican uliyebahatika kufuatana nami toka mwanzo, utakumbuka kuwa tumefanya tafakari ya kina kuhusu asili ya ndoa na familia kama ilivyo kwenye Maandiko Matakatifu na kama Mababa wa Kanisa walivyofundisha kwa nyakati mbalimbali bila kuyatupilia mbali mawazo mazuri ya wana taalimungu wa nyakati zetu. RealAudioMP3
Nakualika sasa kwa vipindi vichache vijavyo tuchukue mtazamo mwingine tupime uwiano uliopo kati ya familia na kazi au kazi na mwanadamu.
Katika kipindi chetu hiki cha kwanza, tukumbushane tena kuwa: kazi ni wajibu au wito ambao chimbuko lake ni Mwenyezi Mungu katika uumbaji. Wajibu huu wa kazi amekabithiwa mwanadamu ambaye hawezi kufikirika nje ya familia.
Masimulizi yote mawili ya uumbaji yaani Mwanzo sura ya kwanza na ya pili mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu amekathiwa kazi zote za uumbaji ili azifanye na kuziendeleza. Ni katika maana hiyo, Mwenye heri Yohane Paulo II katika waraka wake Laborem Exercens, Namba 1, anarudia kusema, mwanadamu aliye sura na mfano hai wa Mungu katika ulimwengu huu amekabidhiwa ulimwengu na yote yaliyoko ndani yake ili ayamiliki na kuyatiisha katika maana hii ameitwa kufanya kazi. Kazi ndicho kipimo cha utu, kipimo cha ubinadamu mwenye mahusiano na binadamu mwingine. La msingi hapa ni kuwa kazi inafanywa na mwanadamu kwa ajili ya mwanadamu.
Kazi sio matokeo ya adhabu ya dhambi ya asili kwani mwaliko wa kufanya kazi ulishakuwepo hata kabla mwanadamu hajaanguka dhambini. Japo matokeo ya dhambi huonekana katika ugumu wa kazi na matumizi mabaya ya maana ya kazi. Ni katika maana hii, Bwana wetu Yesu Kristo alifanya kazi ili kuipa tena kazi heshima yake iliyokuwepo tangu uumbaji. Kazi inapaswa kuwa kwa lengo la kumsaidia mwanadamu na sio mwanadamu ageuke kuwa mtumwa wa kazi. Mahusiano yake na mwanadamu mwingine yasigeuke kuwa chukizo badala ya furaha.
Ndugu msikilizaji, jukumu la ubaba, umama na hata nafasi ya utoto katika familia hudai wajibu fulani, mmoja kwa mwingine, hudai mahusiano na bila mahusiano hayo ya kikazi usitawi wa kifamilia hudumaa na hata kufa. Bila kazi familia hukosa maendeleo yake ya kiroho na kimwili, ni ukweli kuwa wakati mwingine umasikini huzaliwa na hata kulelewa na uvivu.
Ndugu msikilizaji hapa nakualika turejee tena mwaliko wa Mtakatifu Paulo anayesema mtu asiyefanya kazi hana ruksa ya kula chakula ( 2 Kol 3:1-13). Hata hivyo kazi ilete mahusiano mazuri na isiwe sababu kumgeuza mwanadamu mtumwa wa kazi na kuharibu mahusiano mazuri na mwanadamu mwingine.
Kutoka Studio za Radio Vatican ni mimi Padre Raphel Mwanga, wa Jimbo Katoliki la Same, Taasisi ya Ndoa na Familia, Chuo Kikuu cha Kipapa Laterano- Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.