2012-11-12 08:44:38

Jubilee ya miaka 100 ya Ukristo na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani na changamoto zake nchini Nigeria


Askofu mkuu Anthony John Valentine Obinna wa Jimbo kuu la Owerri, Nigeria, anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa namna ya pekee kwa kuwajalia waamini wa Jimbo lake kuweza kuadhimisha Jubilee ya Karne moja tangu waliposikia Habari Njema ya Wokovu, tukio ambalo limewafungulia pia maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliozinduliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita.

Waamini wa Jimbo kuu la Owerri walihubiriwa kwa mara ya kwanza na Wamissionari wa Shirika la Roho Mtakatifu, maarufu kama Holy Ghost, wakitokea eneo la Alsace-Lorraine. Baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia, idadi kubwa ya wamissionari waliwasili nchini Nigeria, wakapandikiza mbegu ya Ukristo, wakaipalilia na sasa katika kipindi cha miaka mia moja imezaa matunda ya idadi kubwa ya Wakristo ambao ni imara katika imani yao, licha ya patashika nguo kuchanika zinazojitokeza hapa na pale. Jimbo kuu la Owerri kwa sasa lina idadi kubwa ya Mapadre na Watawa, kiasi kwamba, linaendelea kushiriki katika kazi ya kimissionari ndani na nje ya Bara la Afrika.

Padre wa kwanza wa Jimbo Katoliki la Owerri, alipadrishwa kunako mwaka 1937 na wa pili alipadrishwa kunako mwaka 1945, hawa ni zawadi kubwa na chemchemi ya miito Jimbo Kuu la Owerri, kwani katika maadhimisho ya Mwaka wa Jubilee, jumla ya Mashemasi ishirini na wanne wamepewa daraja takatifu la Upadre.

Askofu mkuu Obinna anasema kwamba, maadhimisho ya Jubilee ya Karne Moja ya Ukristo Jimbo kuu Owerri ni fursa ya pekee, kuweza kukumbatia na kumwilisha changamoto na fursa mbali mbali, zinazoendelea kutolewa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika: kuiungama imani, kuiadhimisha kwa uchaji mkubwa, kuimwilisha katika maisha kwa kuongozwa na Amri za Mungu pamoja na kuhakikisha kwamba, waamini wanaisali kama njia ya kujenga na kuimarisha uhusiano wao na Kristo pamoja na jirani zao, kwa sifa na utukufu wa Mungu.

Jimbo kuu la Owerri nchini Nigeria linatambua changamoto zinazojitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, inayoufanya ulimwengu kuwa kama kijiji; wanatambua kwamba, kuna tabia ya ukanimungu na watu kupenda mno malimwengu, mwaliko kwa waamini kuyatakatifuza malimwenmgu haya, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Daima wajitahidi kutangaza Ufalme wa Mungu unaojengeka katika misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli. Wanahifadhi ndani mwao, ule Mwanga ambao ni Kristo mwenyewe wanapopambana na malimwengu, ni matumaini yao kwamba, kwa kushikamana na Kristo katika hija ya maisha yao hapa dunia, wataweza kuyashinda malimwengu.

Kwa upande wake, Kardinali mteule John Onaiyekan, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria, amemshukuru kwa namna ya pekee Kardinali Fernando Filoni kwa kufika na kushiriki katika shamra shamra za maadhimisho ya Jubilee ya miaka mia moja ya Jimbo kuu la Owerri.

Anasema, kwa kuteuliwa kwake na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kuwa Kardinali ni changamoto kwake binafsi kuendelea kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kumtumikia Mungu na Kanisa, akimsaidia Khalifa wa Mtakatifu Petro katika kuwaongoza Watu wa Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.