2012-11-12 08:35:10

Jimbo kuu la Owerri, Nigeria lahitimisha Jubilee ya Miaka 100 ya Ukristo


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu, tarehe 10 Novemba 2012, alihitimisha maadhimisho ya Jubilee ya miaka mia moja ya ukatoliki Jimbo kuu la Owerri, nchini Nigeria kwa Ibada ya misa takatifu iliyohudhuriwa na sehemu kubwa ya Familia ya Mungu nchini Nigeria. Ilikuwa ni nafasi ya pekee, kwa ajili ya kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani, kwa wema na ukarimu ambao amewajalia waamini wa Jimbo Kuu la Owerri katika kipindi cha miaka mia moja, tangu waliposikia Injili ya Kristo ikitangazwa masikioni na mioyoni mwao kwa mara ya kwanza.

Kardinali Filoni anasema, miaka mia moja si haba, hata kama ikilinganishwa na Makanisa ambayo yalibahatika kuhibiriwa Habari Njema kwa miaka mingi iliyopita. Kanisa Katoliki Jimbo kuu la Owerri bado ni changa, lina nguvu, ari na mwamko wa pekee, unaojionesha katika ukarimu na uaminifu kwa Kristo na Kanisa lake. Maadhimisho haya ni muhimu kwa ajili ya kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyewakirimia zawadi ya imani kwa takribani miaka mia moja iliyopita.

Ni imani ambayo imepokelewa, ikashuhudiwa, ikaadhimishwa na kumwilishwa kwa moyo wa uchangamfu na watu wa nyakati zile. Hii ndiyo ile imani ambayo, Kanisa limeendelea kuitangaza na kuirithisha kizazi baada ya kizazi.

Ni imani ambayo imafumbata kwa namna ya pekee, Habari Njema ya Wokovu inayomwezesha mwamini kukutana na Kristo Mkombozi wa dunia. Ni imani ambayo imepokelewa na Mitume, wakairithisha kwa waandamizi wao na wale walioipokea wakaendelea kuishuhudia kwa uaminifu mkubwa kwa njia ya maisha yao. Hii ndiyo changamoto iliyoko mbele ya waamini wa Jimbo kuu la Owerri, nchini Nigeria, wakati huu wanapoanza ukurasa mpya baada ya maadhimisho ya Jubilee ya miaka mia moja ya Ukristo Jimboni mwao.

Kardinali Fernando Filoni aliwaalika waamini kusali kwa ajili ya kumshukuru pia Bikira Maria, Mama wa Kanisa na nyota ya Uinjilishaji Mpya, ambaye daima amekuwa ni kielelezo makini cha imani na ufuasi wa Kristo, ili aweze kuwasaidia kuwa kweli ni mihimili ya Uinjilishaji Mpya katika: Familia, Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo na waamini wa dini na madhehebu mbali mbali kwa kujikita katika majadiliano ya kidini na kiekumene, kwani hii pia ni mbinu mpya ya Uinjilishaji Mpya katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Kardinali Filoni anawaalika waamini kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kutangaza Injili ya Kristo kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao kwani Uinjilishaji ni kielelezo cha upendo wa dhati. Waamini wawe na ujasiri wa kushuhudia upya wa imani yao katika maisha yanayobubujika kutoka kwa Kristo, ili waweze kweli kusimama kidete kutangaza na kushuhudia ujumbe wa imani, matumaini na mapendo kwa Familia ya Mungu.








All the contents on this site are copyrighted ©.