Bibi Theresia Nago aomboleza kifo cha mtoto wake Askofu Aloysius Balina wa Jimbo Katoliki
Shinyanga
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameungana
na mamia kwa mamia ya waumini wa Kanisa Katoliki kumzika Askofu Aloysius Balina wa
Jimbo Katoliki Shinyanga yaliyofanyika kwenye Kanisa la Mama wa Huruma, Parokia ya
Ngokolo, mjini Shinyanga.
Rais Kikwete ambaye amekwenda Shinyanga akitokea
Dodoma ambako anaendesha vikao muhimu vya Chama cha Mapinduzi amewasili kwenye Kanisa
hilo kiasi cha saa sita mchana kwa ajili ya mazishi ya Askofu Balina ambaye alifariki
dunia Novemba 6 mwaka huu katika Hospitali ya Rufaa, Mwanza kwa ugonjwa wa saratani.
Mara
baada ya kuwasili Kanisani hapo, Rais Kikwete ametia saini kitabu cha maombolezo na
kujiunga na viongozi wa Kanisa hilo na wa Serikali akiwamo Rais Mstaafu Mheshimiwa
Banjamin Mkapa na Mama Maria Nyerere kushiriki katika mazishi ya kiongozi huyo wa
Kanisa Katoliki.
Kabla ya kutoa salamu zake za rambirambi, Rais Kikwete amesikiliza
salamu za rambirambi kutoka kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, na pia
amesikiliza Waraka uliotangaza kuteuliwa kwa Askofu Mkuu Yuda Thaddeus Ruwa’ichi
kuwa Msimamizi wa Kitume wa Jimbo la Shinyanga hadi atakapoteuliwa Askofu mpya wa
jimbo hilo.
Waraka huo umetolewa na kutiwa saini na Askofu mkuu Protas Rugambwa,
Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu na kusomwa na Askofu
Mkuu Francisco Montecillo Padilla, Balozi wa Vatican nchini tanzania.
Katika
salamu zake zake za rambirambi ambazo amezielekeza kwa Rais wa Baraza la Maaskofu
Tanzania (TEC), Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa na waamini wa Kanisa Katoliki, Rais
Kikwete amemwelezea Askofu Balina kama kiongozi mwadilifu na mchapakazi ambaye hukuchoka
katika maisha yake kutumia nafasi zake mbali mbali alizozishikilia katika maisha yake
kuwasaidia binadamu wenzake.
Rais Kikwete pia ameelezea jitihada ambazo yeye
na Askofu Balina walizifanya katika kusaka fedha za kupanuliwa kwa Hospitali ya Rufaa
ya Bugando iliyoko Mwanza.
Baada ya kutia udongo kwenye kaburi la Askofu Balina
na kuweka shada la maua kwenye kaburi hilo, Rais Kikwete alimpa pole na kumfariji
Bibi Theresia Nago ambaye ni Mama yake mzazi Askofu Balina kabla ya kuondoka Kanisani
hapo.
Askofu Balina alikuwa Askofu wa nne wa Jimbo la Shinyanga nafasi aliyoishikilia
kwa miaka 16 na kabla ya hapo alikuwa Askofu wa Jimbo la Geita kwa miaka 12. Askofu
Balina alikuwa askofu kwa miaka 28 na Padre kwa miaka 41. Aidha, Askofu Balina alikuwa
Mkuu wa Idara ya Afya ya TEC kwa miaka mingi na pia alikuwa Mwenyekiti wa Bodi ya
Wakurugenzi ya Hospitali ya Bugando.