2012-11-09 10:17:32

Uinjilishaji wa awali na ule wa kina ni chanda na pete katika mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo!


Yesu Kristo ni kiini cha Uinjilishaji Mpya unaofanyiwa kazi na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, iwe ni katika Uinjilishaji wa awali au Uinjilishaji Mpya, kwani anabaki kuwa ni Alfa na Omega, nyakati zote ni zake. Kanisa kama Fumbo la Mwili wa Kristo, limepewa dhamana na utume wa kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia.

Ni maneno ya Kardinali Fernando Filoni, Rais wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu, alipokuwa anashiriki katika Kongamano kama sehemu ya maadhimisho ya Jubilee ya miaka mia moja ya Ukristo Jimbo la Owerri, nchini Nigeria. Anasema, Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ulitoa changamoto ya kuanzishwa kwa Makanisa mahalia, ili yaweze kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa na wala si kuwa ni viwanja vya shughuli za kimissionari kama ilivyozoeleka hapo awali kabla ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.

Ulikuwa umefika wakati kwa Kanisa mahalia kuwa mdau mkuu wa Uinjilishaji miongoni mwa watu wake, changamoto endelevu hata katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Kuinjilisha maana yake ni kuwashirikisha na kuwamegea wengine ile furaha ya ndani ya kukutana na Yesu Kristo mkombozi wa dunia, aliyeteswa, akafa na kufufuka, kielelezo makini cha upendo wa Mungu kwa binadamu. Imani hii inamchangamotisha mwamini kuitolea ushuhuda katika uhalisia wa maisha yake, daima akiendelea kutangaza matendo ya Mungu katika ulimwengu mamboleo.

Kardinali Filoni anasema, dhana ya Uinjilishaji Mpya inapata chimbuko lake, miaka kumi baada ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican yaani kunako mwaka 1974, Baba Mtakatifu Paulo wa Sita alipoitisha Sinodi juu ya Uinjilishaji. Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili akaivalia njuga dhana ya Uinjilishaji Mpya na kuipatia kipaumbele cha kwanza katika maisha na mikakati yake ya kichungaji kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. kwa hakika, ndiye muasisi wa neno "Uinjilishaji Mpya".

Yesu Kristo alitumwa na Baba yake wa mbinguni kuja duniani ili kumkomboa mwanadamu, naye kwa upande wake, akawateuwa mitume miongoni mwa wafuasi wake ili kushiriki kwa ukaribu zaidi dhamana ya kutangaza na kueneza Ufalme wa Mungu hadi miisho ya dunia, dhamana inayotekelezwa hadi leo hii na Mama Kanisa. Kwa hakika, Kanisa haliwezi kukaa kitako bila ya kuinjilisha kwani kwa kufanya hivi, litakuwa linasaliti dhamana, wito na utume wake.

Linapaswa kutangaza Habari Njema kwa umakini na ugunduzi mkubwa zaidi, ingawa dhamana hii inakabiliwa pia na changamoto mbali mbali za maisha, ikiwa ni pamoja na madhulumu.

Kardinali Fernando Filoni anahitimisha mchango wake kwa kuwataka waamini kuendeleza majadiliano ya kidini na kiekumene kama njia mufaka ya Uinjilishaji Mpya katika mazingira yao, daima wakiwa wepesi kusoma alama za nyakati, ili kuwaonjesha wengine ile furaha ya kuwa kweli ni wafuasi wa Kristo. Kanisa bado lina changamotishwa kuendelea kuwa ni sauti ya kinabii, inayojikita katika kutafuta mafao ya wengi, haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati, daima likitekeleza wajibu huu msingi kwa njia ya upatanisho wa kweli, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.







All the contents on this site are copyrighted ©.