Benedikto XVI kutembelea wazee kama sehemu ya maadhimisho ya Mwaka wa Wazee na mshikamano
kati ya kizazi na kizazi
Katika maadhimisho ya Mwaka wa Wazee Barani Ulaya na Mshikamano kati ya kizazi na
kizazi, uliotangazwa na Umoja wa Ulaya, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita,
Jumatatu tarehe 12 Novemba 2012, anatarajiwa kutembelea nyumba ya wazee wanaohudumiwa
na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, hapa Roma, kama kielelezo cha mshikamano wa Kanisa
na Wazee.
Baada ya kupokelewa na wenyeji wake, Baba Mtakatifu Benedikto wa
kumi na sita, atawatembelea wanandoa wawili wazee ambao walinusurika kifo wakati wa
tetemeko la ardhi lilipoikumba Haiti, Mwezi Januari, 2010. Atawatembelea wazee wengine
kwenye vyumba sita na baadaye, atakutana na Jumuiya ya Wazeee, watu wanaojitolea pamoja
na wanachama wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio.
Baba Mtakatifu atapata fursa
pia ya kusalimiana na vijana watakaokuwa wamekusanyika nje ya Makazi ya wazee wanaohudumiwa
na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, yenye makao yake makuu hapa mjini Roma.