Watanzania waomboleza kifo cha Askofu Aloysius Balina wa Jimbo Katoliki la Shinyanga
Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Jumanne, Novemba 6, 2012, amelitumia Kanisa Katoliki Tanzania
salamu za rambirambi kuomboleza kifo cha Askofu Aloysius Balina aliyefariki dunia
majira ya saa tano asubuhi, Jumanne tarehe 6 Novemba 2012 kwenye Hospitali ya Rufaa
ya Bugando, Mwanza.
Katika salamu zake za rambirambi kwa Rais wa Baraza la
Maaskofu Tanzania Mshahamu Baba Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais Kikwete amesema:
“Nimepokea kwa mshtuko mkubwa taarifa za kifo cha Mhashamu Baba Askofu Aloysius Balina
ambaye nimeambiwa ameaga dunia asubuhi ya leo kwenye Hospitali ya Rufaa ya Bugando,
Mwanza, kwa ugonjwa wa kansa.” Amesema Rais Kikwete katika salamu zake hizo: “Mhashamu
Baba Askofu Balina alikuwa kiongozi hodari na mwadilifu ambaye siyo tu alichangia
kipekee katika mwenendo mzuri wa kiroho wa waumini wa Kanisa Katoliki bali pia katika
maendeleo ya Watanzania wote kwa jumla.”
“Kifo chake kimetuondolea kiongozi
mwema ambaye tutazikosa busara zake na uongozi wake. Lakini napenda kukuhakishia Mshahamu
Baba Askofu kuwa sisi ndani ya Serikali tutaendelea kutambua na kuthamini mchango
wa Askofu Balina alioutoa kwa nchi yetu katika maisha yake,” amesema Rais Kikwete
na kuongeza:
“Baba Askofu, nakuomba upokee salamu za rambirambi za Serikali
ninayoiongoza na zangu binafsi kufuatia msiba huu mkubwa. Aidha, kupitia kwako, naomba
uwafikishie salamu zangu viongozi na waumini wote wa Kanisa Katoliki kwa kuondokewa
na kiongozi na muumini mwenzao. Naungana nanyi kumwomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa
Rehema, aiweka pema peponi roho ya Marehemu. Amen.”