Rais wa zamani wa Ujerumani, Horst Kohler amepania kutoa msukumo wa kuendeleza Ujasiliamali
Mdogo na wa Kati (SMEs) kwa Afrika Mashariki, ambao unategemewa karibu na asilimia
70 za biashara zinazochipukia hivi sasa katika kanda hiyo. Katika mkutano, kati
yake na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Dk. Richard Sezibera, Berling,
Ujerumani mwishoni mwa wiki, kiongozi huyo wa zamani wa Ujerumani pia ameahidi kuhamasisha
uwekezaji na wajasiliamali wa Ujerumani kuwekeza EAC ili kukuza ujasiliamali mdogo
na wakati. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Sekretarieti ya EAC na Shirika
la Habari Huru la Afrika Mashariki (EANA) kupata nakala yake, Rais huyo wa zamani
ameupongeza mtangamano wa EAC wenye wanachama watano akisema njia hiyo ndiyo bora
zaidi katika mapambano dhidi ya umasiki na kujiletea maendeleo. Wanachama wa EAC ni
pamoja na Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda na Burundi. Kwa upande wake Dk. Sezibera,
alitumia nafasi hiyo kumweleza Rais huyo wa zamani juu ya ziara anayoendelea nayo
mjini Berling na majadiliano muhimu anayoendelea kufanya na maafisa mbalimbali waandamizi
wa serikali ya Ujerumani. Alitoa wito kwa wajasiliamali wadogo na wa kati wa Ujerumani
kuwa na moyo wa kuwekeza katika kanda ya Afrika Mashariki. ‘’Ziara yangu hapa inajikita
zaidi katika kuimarisha mashikamano wetu wa kiuchumi na kihistoria,’’ alifafanua Dk.
Sezibera. Alimshukuru Rais Kohler kwa kuwezesha upatikanaji wa sehemu ya Euro milioni
14 zilizotumika katika kufanikisha ujenzi wa ofisi za makoa makuu ya EAC, mjini Arusha,
Tanzania. Ofisi hizo zinatarajiwa kuzinduliwa rasmi Novemba 28, 2012. Dk. Sezibera
yupo nchini Ujerumani pamoja na mambo mengine kushiriki katika Jukwaa la Kwanza la
Biashara kati ya Ujerumani na EAC ambalo linalenga kuvutia wawekezaji zaidi kutumia
nafasi zilizopo EAC kuwekeza katika nyanja mbalimbali za kiuchumi.