2012-11-07 09:46:50

Vitendo vya jinai vimeongezeka maradufu duniani kutokana na utandawazi, maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja na matumizi ya fedha haramu


Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican, ni kati ya viongozi waliotoa mada wakati wa maadhimisho ya mkutano wa themanini na moja wa Shirika la Interpol, unaotarajiwa kufungwa rasmi Alhamisi tarehe 8 Novemba, 2012.

Wajumbe wa mkutano huu wanapembua kwa kina na mapana changamoto ambazo Jeshi la Polisi linakumbana nazo katika mapambano dhidi ya vitendo vya jinai sehemu mbali mbali za dunia. Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, vitendo vya jinai vimeongezeka maradufu katika mifumo mbali mbali kiasi cha kuhatarisha ulinzi na usalama wa raia na mali zao.

Ni matukio ambayo wakati mwingine yanavuka mipaka ya nchi kutokana na utandawazi, maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja na matumizi ya fedha haramu. Mikakati ya ulinzi na usalama haina budi kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu, utu na heshima yake bila kusahau haki zake msingi kama zilivyobainishwa kwenye Azimio la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa. Ni changamoto kwa Jeshi la Polisi kuhakikisha kwamba, linatafuta sababu za vitendo hivi vya jinai ili hatimaye, kuvikomesha.

Serikali kwa upande wake, hazina budi anasema Askofu mkuu Mamberti kukuza na kuimarisha utawala wa sheria; Bunge na Mahakama zitekeleze nyajibu zao bila kuingiliwa kwa kuzingatia misingi ya: uwajibikaji, ukweli na uwazi na kwamba, sheria ni sawa kwa wote na hakuna mtu ambaye yuko juu ya sheria.

Jumuiya ya Kimataifa inachangamotishwa kuhakikisha kwamba, inaweka mazingira yatakayodumisha utawala wa sheria, kwa ajili ya kutafuta mafao ya wengi bila kusahau mambo msingi yanayopelekea kushamiri kwa ukosefu wa haki ndani ya Jamii husika. Ni vyema zaidi Jamii ikajitahidi kuzuia vitendo vya jinai, kwa kushirikiana na wananchi wenyewe kwani ulinzi na usalama wa raia na mali zao, uko pia mikononi mwao wenyewe.

Jamii isimamie kidete kulinda na kutetea tunu msingi pamoja na kuendelea kutoa malezi bora kwa watoto kuhusu utii wa sheria na mamlaka husika kuanzia ndani ya familia, ambayo kimsingi inapaswa kuwa ni chemchemi ya upendo. Wazazi na walezi anasema Askofu mkuu Dominique Mamberti ni walezi wa kwanza wanaowaonjesha watoto wao haki na msamaha, tunu ambazo ni muhimu sana katika kukuza na kudumisha uhusiano mwema ndani ya Jamii husika.







All the contents on this site are copyrighted ©.