2012-11-07 10:06:00

Toleeni ushuhuda wa umoja katika imani, ili kweli muweze kuwa ni wadau wakuu wa Uinjilishaji Mpya!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ameendelea kusoma alama za nyakati ili kuleta umoja, amani na mshikamano ndani ya Kanisa kwa kutambua kwamba, Liturujia ya Kanisa ni tendo la kumtukuza Mwenyezi Mungu na mwanadamu kutakatifuzwa.

Baba Mtakatifu kunako mwaka 2007 alichapisha Waraka wa Kichungaji uliopembua namna mbali mbali za maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa, kabla ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na mabadiliko haya yakaanza kutumika tarehe 14 Septemba 2007. Katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican, kwenda kwa Wanachama wa Chama cha Mahujaji Kimataifa, Baba Mtakatifu anaendelea kuhimiza umuhimu wa kuendelea kuhifadhi utajiri unaobubujika katika maisha ya imani na sala ya Kanisa kwa kuthamini utajiri wa tunu na maadhimisho mbali mbali ya Liturujia ya Kanisa Katoliki.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema, Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican unaokwenda sanjari na maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ni mwaliko kwa waamini kutolea kwa namna ya pekee, ushuhuda wa umoja katika imani na kwa njia hii, wataweza kuwa kweli ni wadau wakuu wa Uinjilishaji Mpya, utume unaofanyiwa kazi na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Chama cha Mahujaji Kimataifa kutoka Ufaransa, kilihitimisha hija yao mjini Roma kwa maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu, iliyoongozwa na Kardinali Antonio Canizares, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa. Waamini hao walitumia Misale ya Misa Takatifu iliyokuwa inatumika mwaka 1962, iliyokuwa imeidhinishwa na Baba Mtakatifu Yohane wa ishirini na tatu kabla ya kufutwa na mabadiliko yaliyoletwa na Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.