2012-11-07 09:07:34

Marehemu Askofu Balina alisimama kidete kutangaza Injili ya maisha, umoja na mshikamano pamoja na kulitegemeza Kanisa mahalia


Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linaendelea kuomboleza kifo cha Askofu Aloysius Balina wa Jimbo Katoliki Shinyanga kilichotokea hapo tarehe 6 Novemba 2012 kwenye Hospitali ya Rufaa Bugando, Mwanza kutokana na ugonjwa wa Saratani. Mazishi yanatarajiwa kufanyika Jumamosi, tarehe 10 Novemba 2012, Jimboni Shinyanga.

Baraza la Maaskofu bado wanamkumbuka Marehemu Askofu Pascal Kikoti wa Jimbo la Mpanda aliyefariki dunia hivi karibuni, lakini matokeo yote haya ni mapenzi ya Mungu. RealAudioMP3

Hayo yamesemwa na Askofu Michael Msonganzila wa Jimbo Katoliki Musoma, wakati wa mahojiano maalum na Radio Vatican kuhusu kifo cha Askofu Balina. Anasema, ni mtu aliyeyapokea mateso na mahangaiko yake kwa imani kubwa, daima akimtumainia Mwenyezi mungu. Alijitoa bila ya kujibakiza, akatumia nguvu, akili na vipaji mbali mbali alivyokirimiwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kujenga na kuriimarisha Jimbo Katoliki la Geita, kazi ambayo ameifanya kwa takribani miaka kumi na miwili kama Kiongozi mkuu wa Jimbo.

Kasi na mwelekeo huo huo umejionesha pia Jimboni Shinyanga alikowatumikia waamini Jimboni humo kwa muda wa miaka kumi na mitano, muda wa kutosha kabisa kupima mafanikio yaliyojitokeza katika uongozi wa Askofu Balina. Kama mwenyekiti wa Idara ya Afya ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, alikuwa ni kiungo muhimu sana katika maboresho ya huduma ya afya nchini Tanzania, kati ya Kanisa na Serikali chini ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.

Matunda ya mshikamano huu unaolenga mafao ya wengi yamejionesha katika huduma bora zinazotolewa na Hospitali ya Rufaa ya Bugando na tunda lake kuu ni uanzishwaji wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Afya na Sayansi Mwambata, CUHAS. Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, linamshukuru Marehemu Askofu Balina kwa mchango wake mkubwa katika huduma ya afya kwa watanzania.

Askofu Balina, alisimama kidete kupinga mila na desturi zinazokumbatia utamaduni wa kifo kwa dhana ya mauaji ya vikongwe na walemavu wa ngozi, matukio ambayo yalichafua amani na utulivu miongoni mwa watanzania kwa ujumla. Yote haya ni matunda ya baadhi ya watu kuendekeza na kutaka kukumbatia tamaduni na mila potofu ambazo kimsingi zimepitwa na wakati.

Matokeo yake ni kuanzishwa kwa Radio Faraja, ambayo kweli kimekuwa ni chombo cha Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Imeonesha umuhimu wa kusimama kidete kulinda, kutunza na kuendeleza Injili ya maisha, kwa kutambua kwamba, maisha ya binadamu ni matakatifu, kwani binadamu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, anastahili kuheshimiwa na kuthaminiwa.

Marehemu Askofu Balina alikazia umoja, upendo na mshikamano wa dhati miongoni mwa wananchi wote wa Tanzania. Alijitahidi kuendeleza sera ya kulitegemeza Kanisa mahalia kwa kutumia rasilimali iliyokuwepo kwa ajili ya utume na maisha ya Kanisa, changamoto ambayo inapaswa kuendelea kufanyiwa kazi katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Askofu Michael Msonganzila katika mahojiano haya maalum na Radio Vatican anakiri kabisa kwamba, Marehemu Askofu Balina ameonesha unyenyekevu wa pekee katika kuupokea ugonjwa wake na kamwe hakukata tamaa, amekuwa ni mwalimu ambaye ameacha fundisho la kuthamini mateso katika maisha. Apumzike kwa Amani. Amina.







All the contents on this site are copyrighted ©.