2012-11-07 08:29:39

Kanisa Barani Afrika bado lina wajibu wa kusikiliza kwa makini sauti ya Kristo!


Mheshimiwa Dr. Thèodore C. Loko, Balozi wa Benin mjini Vatican, hivi karibuni amezindua vitabu viwili vinavyoonesha hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita nchini Benin wakati wa kuwasilisha matunda ya Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika, hapo mwaka 2011 sanjari na kumbu kumbu ya ushirikiano wa Kidiplomasia kati ya Vatican na Benin, tukio ambalo limehudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Kanisa kutoka Vatican na Benin. RealAudioMP3

Hii ni kumbu kumbu endelevu, changamoto na dhamana ya Kanisa Barani Afrika kuendelea kuisikiliza kwa umakini mkubwa sauti ya Kristo, hasa wakati huu ambako kuna myumbo wa uchumi, kinzani, migogoro na kumong’onyoka kwa tunu msingi za maisha adili na utu wema kutokana na madhara ya utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Madhara haya yanajionesha katika medani mbali mbali za maisha ya watu wengi duniani na Afrika kwa sasa wanaanza kuonja makali yake, lakini ikumbukwe kwamba, waathirika wakubwa ni maskini na familia zao.

Ni changamoto inayotolewa na Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum, alipokuwa anachangia mada kwenye tukio hili ambalo limeacha kumbu kumbu kubwa kwa Familia ya Mungu Barani Afrika. Anasema, dalili za myumbo wa uchumi kimataifa zilianza kujionesha kwa namna ya pekee Nchini Marekani na Ulaya kunako mwaka 2008. Haya ni matokeo yanayopata chimbuko lake kutokana na sera za kukumbatia utamaduni wa kifo, leo hii kuna idadi kubwa ya wazee wanaohitaji hifadhi za kijamii, ikilinganishwa na idadi ya watoto wanaozaliwa kwenye Familia za Nchi za Ulaya. Madhara yake yanaendelea kujionesha hata katika medani za kijamii, kimazingira na kitamaduni.

Matokeo yake kwa Bara la Afrika anasema Kardinali Robert Sarah ni uwapo wa wimbi kubwa la wale wanaodaiwa kuwa ni wawekezaji Barani Afrika, wanaoendelea kukwapua maeneo makubwa ya ardhi, bila kuzingatia mafao ya wengi na matokeo yake ni wasi wasi na woga wa mustakabali wa Bara la Afrika kwa siku za usoni. Kuna wahamiaji wengi kutoka Asia, Uarabuni na Ulaya wanaohamia Barani Afrika, hali ambayo imejionesha kwa namna ya pekee kwa wahamiaji kutoka Ureno kwenda Angola na Msumbiji.

Licha ya mwelekeo huu hasi Barani Afrika, lakini pia kumekuwepo na dalili nzuri za kukua na kuimarika kwa uchumi kwa nchi nyingi za Kiafrika, licha ya mtikisiko wa uchumi kimataifa. Nchi nyingi Barani Afrika zina matumaini kwamba, zinaweza kuvuka balaa la umaskini wa kukithiri miongoni mwa watu wake. Kuna dalili za amani na utulivu kwa nchi nyingi za Kiafrika, ingawa bado migogoro ya kivita, kijamii na kidini inaendelea kusikika kutoka sehemu mbali mbali za Bara la Afrika.

Athari za ugonjwa wa Ukimwi; vita huko DRC, Mali, Somalia, Vitendo vya kigaidi: Nigeria, Kenya na Tanzania ni matukio yanayoendelea kuchafua kwa kiasi kikubwa amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa. Kuna haja kwa Serikali mbali mbali Barani Afrika kuhakikisha kwamba, zinalinda na kudumisha uhuru wa kuabudu, uhuru wa dhamiri, haki msingi za binadamu na utawala wa sheria.

Kardinali Sarah anakumbusha kwamba, “Madhulumu na Ukristo ni sawa na Mwana na Mbereko”, hali ambayo imejionesha tangu mwanzo wa Ukristo, lakini ifahamike kuwa, damu ya mashahidi imekuwa ni mbegu ya Ukristo. Kanisa Barani Afrika halina budi kuisikiliza sauti ya Kristo inayowaalika kutekeleza dhamana yake, kama anavyo bainisha Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika Waraka wake wa kichungaji, Africae Munus, Dhamana ya Afrika.

Hakuna maendeleo ya kweli yasiyozingatia mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili; yasiyotambua na kuheshimu uwapo wa Mungu wala kushughulikia mafao ya wengi na ustawi wa watu wa Bara la Afrika. Inasikitisha kuona kwamba, kuna Mataifa Makubwa, Mashirika ya Kimataifa na Makampuni makubwa yanayokimbilia Barani Afrika yakiwa na nguvu ya fedha, kiasi cha kutetetemesha mawazo ya wanasiasa na hivyo kujikuta wanatelekeza dhamana na wajibu wao kwa kukumbatia sera, mawazo na tamaduni ambazo hazina mafao wala tija kwa maendeleo na ustawi wa Bara la Afrika.

Fedha, na ukuaji wa uchumi usiozingatia maadili na utu wema, ni kulitumbukiza Bara la Afrika katika matatizo makubwa kwa sasa na kwa siku za usoni. Maendeleo lazima yaguse mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Maendeleo yakuzwe hatua kwa hatua, kwa kuwekeza katika sekta ya elimu, utu na heshima ya binadamu sanjari na kutambua dhamana na umuhimu wa kazi, kama utimilifu wa mtu mzima.

Afya, utunzaji bora wa mazingira, utulivu, haki, amani, umoja na mshikamano wa kitaifa; majadiliano ya kidini, kisiasa na kiekuemene; ushiriki wa wananchi katika kupanga, kuamua na kutekeleza masuala yanayogusa maisha yao, bila kuwasahau wanyonge na maskini. Kuna nchi kadhaa Barani Afrika zimekuwa kweli ni mfano wa kuigwa kwa Jumuiya ya Kimataifa, changamoto kwa nchi nyingine kujibidisha kuboresha hali ya maisha ya watu wao.

Bara la Afrika linachangamotishwa na Mama Kanisa kusikiliza kwa makini sauti ya Kristo na kutekeleza dhamana ya Kanisa katika Uinjilishaji Mpya, mwaliko kutoka kwa Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya ambayo imekwenda sanjari na Maadhimisho ya Jubilee ya miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na Mwaka wa Imani, unaopania kwa namna ya pekee, kuwajengea uwezo waamini ili waweze kutolea ushuhuda imani wanayoungama, adhimisha, ishi na kusali.

Wakati wa maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, nchi nyingi za Kiafrika zilikuwa zinajipatia uhuru wake, Kanisa likawa kweli ni mhimili mkuu wa maendeleo endelevu ya watu wa Afrika, kwa kuwapatia matumaini ya leo na kesho iliyo bora zaidi kwa njia ya huduma bora katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Kanisa Barani Afrika, likapewa changamoto ya kuwa ni la Kimissionari ili kujitosheleza kwa rasilimali watu katika mchakato wa Uinjilishaji kwa ajili ya Bara la Afrika na Ulimwengu kwa ujumla wake.

Kanisa Barani Afrika bado lina dhamana ya kuwatangazia watu Habari Njema, kwa kuendeleza dhamana ya Kanisa kama Familia ya Mungu inayowajibika, kwa kukuza na kudumisha, umoja na mshikamano wa Kikanisa. Kanisa halina budi kuwa karibu na watu katika hija ya maisha yao ya kila siku: wakati wa raha na karaha, wakati wa furaha na majonzi, daima likijitahidi kutangaza Injili ya Upendo.

Kanisa Barani Afrika linapaswa kujikita katika mchakato utakaoliwezesha kuwa kweli ni sauti ya kinabii, inayopania kukuza na kudumisha haki, amani na upatanisho. Amani inafumbatwa katika nguzo ya: ukweli, uhuru, haki na upendo, kama alivyobaianaisha Baba Mtakatifu Yohane wa Ishirini na Tatu, katika Waraka wake wa Kichungaji, Amani Duniani “Pacem in Terris”

Kardinali Robert Sarah anahitimisha mchango wake kwa kusema kwamba, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ana matumaini makubwa kwa Kanisa la Bara la Afrika, yanayofumbatwa ndani ya tunu msingi za kiutu na maisha ya kijamii. Familia ya Mungu Barani Afrika, isikatishwe tamaa kuzionesha na kuzimwilisha tunu hizi kama sehemu ya mchango wake kwa maendeleo na ustawi wa mwanadamu.








All the contents on this site are copyrighted ©.