2012-11-05 10:44:17

Mkutano wa 81 wa Interpol waanza mjini Roma


Waziri wa mambo ya ndani wa Italia Annamaria Cancellieri, Jumatatu, tarehe 5 Novemba 2011, amefungua mkutano wa mwaka wa themanini na moja wa Interpol unaoongozwa na kauli mbiu "changamoto kwa Jeshi la Polisi katika kukabiliana na ghasia katika ulimwengu mamboleo", kwa kuzitaka nchi wanachama wa Interpol, kuhakikisha kwamba, zinazidisha na kuimarisha ushirikiano katika mapambano dhidi ya vitendo vya jinai.

Mkutano mkuu wa Interpol unawahusisha Mawaziri wa mambo ya ndani ya nchi na Wakuu wa Jeshi la Polisi kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wanaojumuika kwa pamoja ili kupembua matatizo ya usalama wanayokabiliana nayo katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Mapambano dhidi ya vitendo vya jinai yanakwamishwa wakati mwingine kutokana na mipaka na sheria za nchi, lakini wahalifu wanajikuta wakipeta hata kuvuka mipaka ya nchi husika kwa kuendelea kila siku kutafuta mbinu ya kukwepa mkondo wa sheria.

Kutokana na vitisho na ongezeko la vitendo vya jinai, mkutano mkuu wa Interpol kwa mwaka 2012 umekuwa na ushiriki mkubwa kutoka kwa Mawaziri wa mambo ya ndani ya nchi 103; nchi 169 zinawakilishwa; kuna jumla ya wawakilishi 1,100 na wakuu wa Jeshi la Polisi 81 kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Mada ambazo zinafanyiwa kazi kwa sasa hadi hapo tarehe 8 Novemba 2012 ni: wahamiaji haramu; wizi kwa njia ya mitandao; ugaidi, uharamia baharini, mapambano dhidi ya vitendo vya jinai, biashara haramu ya nyara za taifa na fujo pamoja na ghasia mijini.







All the contents on this site are copyrighted ©.