Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kuzindua Mwaka wa Imani kwenye Kanisa kuu la
Mt. Yosefu, Jimbo kuu la Dar es Salaam, 9 Novemba 2012
Mwaka wa Imani ulifunguliwa rasmi na Baba Mtakatifu Benedikto wa XVI mnamo tarehe
11/10/2012. Katika kuufungua rasmi Mwaka wa Imani, Papa Benedikto aliadhimisha Ibada
ya Misa maalum katika Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican. Kila kanisa mahalia
litapaswa pia kuadhimisha ibada maalum kwa ajili ya kufungua na kufunga Mwaka huo.
Mwaka huu wa Imani utafikia kilele chake tarehe 24 Novemba 2013 katika Sherehe ya
Kristo Mfalme.
Mwaka wa Imani unakwenda sanjari na maadhimisho ya Jubilee ya
Miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, kumbu kumbu ya miaka ishirini, tangu
Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili alipochapisha Katekisimu ya Kanisa Katoliki pamoja
na maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu Uinjilishaji Mpya kama nyenzo ya kueneza
Imani ya Kikristo.
Hapa Tanzania, Baraza la Maaskofu Tanzania limepanga kufungua
rasmi kitaifa Mwaka wa Imani tarehe 9/11/2012 kwa Ibada ya Misa Takatifu itakayoadhimishwa
katika Kanisa kuu la Mtakatifu Yosefu, Jimbo kuu la Dar – es – Salaam saa 10.30 jioni.
Ibada hiyo inatarajiwa kuhudhuriwa na baadhi Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania.
Baada
ya ufunguzi huu wa Kitaifa, kila Jimbo litapanga ratiba ya kufungua Mwaka wa Imani
Kijimbo na kupanga mikakati mbali mbali katika kuuadhimisha Mwaka huu wa Imani.
Mambo
muhimu ya kufanya katika Mwaka huu wa Imani: Ni pamoja na kutafakari mwito unaoandamana
na Barua ya Kitume ya Baba Mtakatifu katika Mwaka wa Imani iitwayo: Mlango wa Imani.
Maneno haya Mlango wa Imani yamechukuliwa katika Biblia Takatifu Kitabu cha Matendo
ya Mitume sura 14 aya 27 kwamba, Mlango wa Imani umefunguliwa kwa Mataifa yote.
Kauli
mbiu ya kuadhimisha Mwaka wa Imani ni “Uinjilishaji Mpya kwa ajili ya Kueneza Imani
ya Kikristo”. Hivi tunaalikwa kuangalia katika nyanja mbali mbali ni mbinu zipi zitasaidia
katika Uinjilishaji mpya katika kueneza Imani ya Kikristo. Tukianza na Familia, Jumuia
Ndogo Ndogo za Kikristo, Jumuia za Malezi, Vigango, Parokia na Vyama vya Kitume.
Umetolewa wimbo maalumu wenye maneno: Ninasadiki, Bwana, utuongezee Imani.
Wimbo huu ni maombi ya kiulimwengu ya binadamu wote na mataifa yote, watu wa kila
aina na hali, watu wa nyakati zote; ni maombi ya wanadamu kwa Muumba wao, ili Mwanga
wake uwaelekee wanapoungana na Bwana Yesu Kristo, Mama Bikira Maria pamoja na watakatifu
wote katika wajibu wa binadamu wote kwa Muumba wao wa kujitakatifuza na kuyatakatifuza
malimwengu.
Siri kubwa ya mafanikio yao katika kuelekea Mbingu Mpya na Dunia
Mpya ni kumwomba Roho Mtakatifu atawale pote wakijiaminisha katika Msalaba wa Yesu
Kristo Mfufuka ili kuyamaliza matatizo yaletwayo na usiku wa maovu ya dunia hii na
kuamkia upya wa uzima wa ki-Mungu.
Ni mwaliko pia kwa wataalamu wetu wa muziki
wa Kanisa kuyatumia maneno ya wimbo huu na kutunga nyimbo katika mahadhi yetu hapa
Tanzania zitakazotusaidia kuuishi Mwaka wa Imani kwa ushiriki hai.
Heri ya
Mwaka wa Imani
Na Padre Paterni Patrick Mangi Katibu Mtendaji, Idara
ya Liturujia Baraza la Maaskofu, Tanzania.