2012-11-03 09:21:14

Pax Christi yamtunukia Tuzo la Amani Kardinali mteule John Onaiyekan kwa kusimama kidete kulinda na kudumisha majadiliano ya kidini


Kardinali mteule John Onaiyekan, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria, hivi karibuni amekabidhiwa Tuzo la Amani kutoka kwa Shirika la Amani Kimataifa, Pax Christi, kutokana na mchango wake mkubwa katika kukuza na kudumisha majadiliano ya kidini na waamini wa dini mbali mbali Barani Afrika, lakini kwa namna ya pekee, na waamini wa dini ya Kiislam, ili kudumisha misingi ya haki, amani, utulivu na maendeleo endelevu, yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Tukio hili ambalo limefanyika kwenye Makao Makuu ya Pax Christi, limehudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Kanisa na Serikali na Jumuiya ya Kimataifa. Viongozi wote hawa wametambua mchango wa Kardinali mteule Onaiyekan katika kukuza majadiliano ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam nchini Nigeria, mahali ambapo kwa sasa umegeuka kuwa ni "Uwanja wa Fujo" kutokana na vitendo vya kigaidi, vinavyoendelea kuhatarisha amani, utulivu, umoja na mstakabali wa wananchi wa Nigeria katika ujumla wao.

Kardinali mteule Onaiyekan, licha ya vurugu zote hizi, bado hajakata tamaa na daima ameendelea kusimama kidete: kulinda, kutetea na kudumisha misingi ya haki, amani, majadiliano ya kidini; fadhila ambazo zimemwezesha kutunukiwa Tuzo ya Amani na Pax Christi kwa Mwaka 2012. Tuzo ya Amani hutolewa kwa watu ambao wameonesha jitihada za pekee kabisa katika kukuza na kudumisha haki, amani, majadiliano badala ya kuendekeza vurugu na uvunjifu wa amani kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Kardinali mteule Onaiyekan anayetarajiwa kusimikwa rasmi hapo tarehe 24 Novemba, 2012 hapa mjini Vatican, amewashukuru viongozi wa Pax Christi, kwa kumpatia heshima kubwa kwa kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kuchochea umoja na mshikamano; upendo na amani, kwa kutambua kwamba, leo hii ulimwengu umekuwa kama Kijiji; kila mtu anaguswa na yale yanayotokea hata mbali kabisa ya nchi yake.







All the contents on this site are copyrighted ©.