2012-11-03 07:50:27

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani ni changamoto ya: Kusikiliza na kutekeleza utume wa Kanisa katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya


Askofu mkuu Luis Antonio Tagle wa Jimbo kuu la Manila, Ufilippini ni kati ya Makardinali wapya walioteuliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kuongeza nguvu katika huduma ya kufundisha, kutakatifuza na kuwaongoza Watu wa Mungu, inayotolewa na Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa Kanisa la Kiulimwengu; utume ambo unasimikwa katika mshikamano wa umoja na upendo mkamilifu.Kutujuvya zaidi ndani ya viunga vya Radio Vatican ni Sr. Gisela Upendo Msuya. RealAudioMP3

Kardinali Mteule Luis Antonio Tagle anapenda kuchukua nafasi hii kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu na kwa namna ya pekee baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa kumpatia dhamana ya kushirikiana naye kwa karibu katika kuliongoza Kanisa. Kuteuliwa kwake ni changamoto endelevu kwa Kanisa Barani Asia kuzidisha juhudi za Uinjilishaji Mpya unaojikita katika majadiliano ya kidini na kiekuemene, kwa kutambua na kuthamini mchango mkubwa unaoendelea kutolewa na Kanisa Katoliki nchini Ufilippini.

Kila mwamini anapaswa kutambua dhamana ambayo amekabidhiwa na Mama Kanisa ya kujikita kwa njia ya ushuhuda wa maneno lakini zaidi wa matendo yake katika utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia.

Kardinali mteule Luis Antonio Tagle katika barua yake ya kichungaji kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, utakaohitimishwa kwa maadhimisho ya Siku kuu ya Kristo Mfalme hapo tarehe 24 Novemba 2013 ni mwaliko na changamoto ya kuadhimisha kwa ari na moyo mkuu zaidi, ile zawadi ya imani waliyoipokea kama kito cha thamani kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kwa kuiishi na kuitangaza kwa njia ya ushuhuda wa maisha yenye furaha ya kukutana na Kristo.

Mwaka wa Imani una utajiri mkubwa unaowasukuma waamini kwa namna ya pekee, kujichotea utajiri unaoendelea kububujika kutoka katika Nyaraka Kumi na Sita za Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican; Muhtasari wa Imani ambayo waamini wanakiri, adhimisha, wanajitahidi kuiishi na kuisali kama inavyofafanuliwa na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki. Ni changamoto ya kuendeleza Mapokeo ya Kanisa kabla na baada ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican kama alivyofafanua Baba Mtakatifu Yohane wa Ishirini na tatu wakati wa kuzindua maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.

Maadhimisho ya Mwaka Imani uwawezeshe waamini kuzama na kuibua utajiri ambao umefichika katika Nyaraka hizi ambazo kwa hakika ni dira na mwongozo kwa maisha na utume wa Kanisa katika ulimwengu mamboleo. Hizi ni jitihada za Mama Kanisa katika kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji Mpya unaopania kuamsha tena Imani ili kukabuiliana na changamoto, matatizo na fursa mbali mbali zinazojitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Licha ya dhana ya ukanimungu kuendelea kushamiri kati ya watu, lakini bado kuna kundi kubwa la Vijana na Maskini wa Roho wenye kiu ya kutaka kusikia Neno la Mungu likitangazwa kwa ari na nguvu mpya maishani mwao, kwa kusoma alama za nyakati, kutafuta mbinu muafaka, kusikiliza na kuendelea kujikita katika maisha na utume wa Kanisa.

Kardinali mteule Luis Antonio Tagle, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Manila katika barua yake ya kichungaji kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani anabainisha kwamba, Mwenyezi Mungu ndiye anayemfungulia mja wake mlango wa mahusiano na umoja unaojikita katika Fumbo la Utatu Mtakatifu ili kuanza hija ya maisha ya kiroho inayoyojidhihirisha katika Kanisa ambalo kimsingi ni: Jumuiya ya Waamini na Tunda la kazi ya Roho Mtakatifu, inayowahamasisha Wafuasi wa Kristo kujitoa kimasomaso kuendeleza utume wa Kimissionari kwani Kanisa lipo kwa ajili ya Kuinjilisha.

Ili waamini waweze kuishuhudia Imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, hawana budi kwanza kabisa kuwa na ufahamu wa kina kuhusu Biblia, dhamana inayoweza kuboreshwa kwa kukazia utume wa Biblia miongoni mwa waamini, ili kila mtu aweze kuonja utamu wa Neno la Mungu ambalo linapaswa kuwa ni mwanga na taa inayoyaangazia mapito ya waamini katika hija ya maisha yao hapa duniani.

Waamini waifahamu kwa kina na mapana Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki. Waendelee kuvumbua utajiri wa Mafundisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na Nyaraka mbali mbali ambazo zinaendelea kutolewa na Viongozi wa Kanisa. Mwaka wa Imani, uwawezeshe waamini kuadhimisha Sakramenti za Kanisa kwa furaha, imani na uchaji na kamwe lisiwe ni jambo la mazoea ya kushiriki Liturujia na Maisha ya Sala.

Mwaka wa Imani uoneshe mwamko na ari kubwa zaidi ambayo ni matunda ya toba na wongofu wa ndani, unaopania kwa namna ya pekee, kujenga utakatifu kama kielelezo cha juu kabisa cha uhusiano kati ya Mwamini na Muumba wake. Yote haya yajidhihirishe katika maisha adili, haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Waamini wajitahidi kukuza na kudumisha Umoja wa Kikanisa kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa; daima wakijitahidi kujenga Ufalme wa Mungu unaosimikwa katika misingi ya haki, amani na utulivu.








All the contents on this site are copyrighted ©.