2012-11-02 13:54:51

"Watanzania msiwe vibaraka wa kuchochea vurugu na ghasia!


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa hakuna mtu yoyote ama kikundi chochote cha watu kitakachoruhusiwa kuvuruga amani na utulivu wa Tanzania. Aidha, Rais Kikwete amewataka wananchi kuepukana na mtego wa kufanywa kaseti na gramafoni ya watu wengine katika mchakato wa sasa wa kutoa maoni kwa ajili ya Katiba Mpya ya Tanzania.

Rais Kikwete ameyasema hayo Alhamisi, Novemba Mosi, mwaka 2012, wakati alipozungumza na wananchi wa Wilaya ya Arumeru, Mkoa wa Arusha, baada ya kuwa amefungua rasmi hospitali ya Serikali ya Olturumet nje kidogo ya mji wa Arusha.

Rais Kikwete amewaambia wananchi hao kuwa mambo ya fujo ambayo yamejitokeza nchini katika wiki za karibuni ni mambo ya aibu na ya kuchukiza. “Yaliyotokea na yanayoendelea kuonyesha dalili za kujitokeza ambako watu wanafanya fujo ni mambo ya aibu na ya kuchukiza. Wapo watu wanaotumiwa ili kuvuruga amani ya nchi yetu kwa sababu siyo kila mtu anafurahia utulivu ulioko hapa nchini.”

Ameongeza Rais Kikwete: “Lakini wananchi msiwe na wasiwasi, sisi tutashughulika na hawa watu na kwa kweli hakuna mtu yoyote ama kikundi cha watu kitakachoruhusiwa kuvuruga amani na utulivu wa Tanzania.” Hivi karibuni hasa katika Jiji la Dar es Salaam na Zanzibar, zimejitokeza fujo zilizopelekea watu kadhaa kutiwa mbaroni na Polisi na kufikishwa mahakamani.

Kuhusu mchakato wa Katiba Mpya, Rais Kikwete amewataka wananchi kuwa huru kutoa maoni yake mbele ya wajumbe wa Tume ya Katiba. Amewaambia wananchi: “Toeni maoni yenu kwa uhuru kabisa, msitishwe na mtu yoyote. Jambo moja tu nataka kulisema – msigeuke kuwa kaseti ama gramafoni za kutangaza na kunadi maoni ya mtu mwingine. Hii ndiyo njia itakayotuwezesha sote kupata Katiba nzuri na itayoitumikia nchi yetu kwa miaka mingi ijayo.”









All the contents on this site are copyrighted ©.