Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican katika tahariri yake juma hili, anauangalia
kwa namna ya pekee Mwezi Novemba, ambao umetengwa rasmi na Mama Kanisa kwa ajili ya
kuwakumbuka na kuwaombea waamini marehemu. Ni mwaliko wa kuyainua macho mbinguni kwa
imani na matumaini juu ya ufufuko wa wafu na uzima wa milele ijayo.
Macho
ya waamini yanatamani kuiona Jumuiya ya wale waliokombolewa, yaani watakatifu wanaoendelea
kufurahia utukufu wa Mungu katika maisha ya uzima wa milele; waamini wanatumaini la
kuonja umoja wao katika maisha ya kiroho, waamini wanapoendelea na hija ya maisha
yao kuelekea mbinguni. Hii ndiyo maana ya Sherehe ya Watakatifu Wote, ambayo Mama
Kanisa ameiadhimisha hapo tarehe Mosi, Novemba.
Waamini wanaonesha mshikamano
wao wa kiroho na waamini waliotangulia mbele za haki kwa kuwakumbuka katika sala na
matumaini. Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya, katika ujumbe wao
kwa Watu wa Mungu wanasema kwamba, Yesu alipokutana na yule mwanamke Msamaria alijionesha
si tu kwamba, ni mtu anayetoa maisha, bali zaidi sana ni mtu anayemkirimia mwanadamu
maisha ya uzima wa milele.
Padre Lombardi anasema kwamba, zawadi hii kutoka
kwa Mwenyezi Mungu hajikiti katika ahadi ya maisha bora hapa ulimwenguni, lakini ni
ujumbe unaolenga katika hatima ya maisha ya mwanadamu baada ya kifo, yaani muungano
mkamilifu na Mwenyezi Mungu, jambo ambalo waamini wanalisubiri hadi utimilifu wa dahali.
Ujumbe wa Mababa wa Sinodi unaendelea kukazia kwamba, kwa wale ambao wamewekwa
wakfu kwa ajili ya Mungu na jirani, katika nadhiri ya ufukara, useja na utii, wanapaswa
kuwa kweli ni kielelezo cha matumaini ya maisha ya binadamu yanayopita mipaka ya kifo.
Ni wito angavu lakini una madai yake makubwa!
Utekelezaji wa majukumu hapa
duniani ni haki na jambo muhimu kabisa, lakini hauna budi kulishwa na kuchangamotishwa
na tumaini linaloelekea kwenye mbingu na dunia mpya. Padre Federico Lombardi anahitimisha
tahariri yake kwa kusema kwamba, bila tumaini hili, dhamana ya Uinjilishaji wa awali
ingegonga mwamba na wala kusingalikuwepo na ndoto kuhusu Uinjilishaji Mpya. Ni vyema,
kwa waamini kuviinua vichwa vyao, ili kumwangalia Kristo anayekuja akiwa na jeshi
kubwa la watakatifu.