2012-11-02 14:19:52

Mwilisheni Injili ya Upendo kwa kuwahudumia maskini, wagonjwa na wote wanaokosa hakimsingi za kijamii!


Kardinali Thèodor Adrien Sarr, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dakar, Senegal, katika maadhimisho ya Sherehe ya Watakatifu wote, anaendelea kuwaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kujitahidi katika hija ya maisha yao hapa duniani kuhakikisha kwamba, wanamwilisha Injili ya Upendo kwa waathirika wa majanga asilia, umaskini, magonjwa, ujinga na ukosefu wa misingi ya haki jamii.

Ni sherehe inayopaswa kuacha chapa ya kudumu katika maisha ya waamini, kwani kila mwamini anachangamotishwa na Mama Kanisa kuwa ni mtakatifu, mwaliko wa kwanza kabisa kutolewa na Kristo mwenyewe. Maisha na majina ya watakatifu yasibaki kwenye Kalenda zilizotundikwa ukutani au vitabu vilivyofichwa kwenye makabati, bali yawe ni maisha halisi yanayojionesha katika hija ya waamini hapa duniani.

Ni safari ya kiroho inayopaswa kufanyika kwa kukumbatia kwa namna ya pekee: unyenyekevu, uvumilivu na utu wema, daima wakipania kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati. Fadhila hizi zinapaswa kuwa ni chimbuko la upatanisho, msamaha na furaha ya ndani inayobubujika kutoka kwa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu, limbuko lao waliolala katika maisha ya uzima wa milele.

Kardinali Sarr kwa namna ya pekee, ameichangamotisha Serikali ya Senegal kuhakikisha kwamba, inawatia mbaroni na kuwafikisha kwenye mkondo wa sheria, watu waliofanya vitendo vya kihuni kwa kubomoa makaburi ya Wakristo nchini Senegal hivi karibuni, kwani makaburi ni maeneo matakatifu yanapaswa kuheshimiwa na kuhifadhiwa na kila raia, kwani hii ni nyumba ya kila mwanadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.