2012-11-01 09:02:42

Yesu Kristo Mwanga wa Mataifa ajioneshe katika: Liturujia, Neno la Mungu, Kanisa na katika Ulimwengu


Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya katika Ujumbe wao kwa Familia ya Mungu wanabainisha kwamba, fursa mbali mbali zinazotolewa na Mama Kanisa katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na Miaka ishirini tangu Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili, alipochapisha Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, ziwe ni fursa makini katika azma ya Uinjilishaji Mpya.

Kwa namna ya pekee, Mababa wa Sinodi wanakazia umuhimu wa Liturujia katika maisha na utume wa Kanisa, kama chechemi ya imani na mahali ambapo panapaswa kupewa kipaumbele cha pekee katika kuiungamana, kuitangaza na kuimwilisha Imani ya Kikristo. Liturujia ya Neno la Mungu ilete changamoto ya pekee kwa waamini kupenda kulitafakari, kulisoma na kulimwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha yao.

Daima wakumbuke kwamba, Neno hili halina budi kupokelewa katika hali ya utulivu, kumwilishwa kwa njia ya huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili kutambua ile sura ya Kristo mteswa inayojionesha miongoni mwa ndugu zake walio wadogo.

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Askofu Salutaris Libena wa Jimbo Katoliki Ifakara ambaye alikuwa ni kati ya Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya anabainisha umuhimu wa Liturujia katika maisha na utume wa Kanisa kwa kufanya rejea kutoka katika Waraka wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani "Porta Fidei" "Mlango wa Imani" kwamba, Mwaka huu, waamini wajitahidi kumtambua Kristo Mwanga wa Mataifa anayejionesha kwa namna ya pekee kabisa katika Liturujia, Maandiko Matakatifu, Kanisa na Katika Ulimwengu.

Kimsingi huu ni muhtasari wa Mafundisho Makuu ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican yanayofumbatwa katika Nyaraka zifuatazo: Liturujia, Maandiko Matakatifu, Kanisa na Ulimwengu. Kwa njia ya Liturujia, waamini wanaweza kumtukuza, kumshukuru, kumwomba, kumsifu na kumwabudu mwenyezi Mungu kwa njia ya Neno lake, Sakramenti za Kanisa, Matendo ya Huruma, Umoja na Mshikamano miongoni mwa Wafuasi wa Kristo. Waamini wakiweza kuitambua na kuiishi Liturujia ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.