Michoro ya Kikanisa cha Sistina ni mwaliko wa kusali na kutafakari ili kugundua utajiri
unaofumbatwa katika michoro hii
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumatano tarehe 31 Oktoba, 2012 ameongoza
waamini katika maadhimisho ya Masifu kwa ajili ya Watakatifu Wote sanjari na Jubilee
ya miaka mia tano tangu Baba Mtakatifu Giulio wa Pili alipozindua Michoro iliyopo
kwenye Kikanisa cha Sistina.
Tukio hili la kihistoria na kisanii limeadhimishwa
katika Liturujia kwa kutambua umuhimu wa Kikanisa cha Sistina katika maisha na utume
wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Michoro iliyopo inapata chimbuko lake katika Liturujia
ya Kanisa na uzuri wake unajionesha kwa namna ya pekee kabisa, kwani maadhimisho ya
Kiliturujia yanakwenda sanjari na uzuri unaogusa undani wa maisha ya mwamini kiroho.
Kwa maneno machache anasema Baba Mtakatifu, michoro ya Kikanisa cha Sistina ni mwaliko
wa kusali na kufanya tafakari ya kina ili kugundua utajiri unaofumbatwa katika michoro
hii.
Baba Mtakatifu anasema, Liturujia ya Neno la Mungu inawakumbusha waamini
kwamba, Ahadi za Agano la Kale zilizotolewa na Mwenyezi Mungu zinatoa kipaumbele cha
kwanza kwa waamini hao kujenga umoja na mshikamano: Mwenyezi Mungu na Kristo wakiwa
ni kiini cha maadhimisho yao. Michoro iliyoko kwenye Kikanisa cha Sistina inaonesha
Jumuiya ya Watakatifu, Bikira Maria, Mama wa Matumaini, Yesu Kristo Mkombozi wa Ulimwengu
akiwa kati kati kabisa ya michoro yote, hali akiwa amezungukwa na Jeshi la Watakatifu.
Msanii
Michelangelo alipewa dhamana ya kuchora kwenye Kikanisa cha Sistina na Papa Giulio
wa Pili, kazi ambayo aliitekeleza kwa kipindi cha miaka minne, kuanzia mwaka 1508
hadi mwaka 1512, michoro ambayo inamguso wa pekee kwa mtu anayetembelea Kikanisa hiki.
Ni michoro iliyoleta mabadiliko makubwa katika historia ya sanaa ya Italia
na kwa Bara la Ulaya katika ujumla wake, kwani huu ni mwanga unaoiangazia dunia kutokana
na uzuri wake. Ni mwanga wa Mungu unaoangazia michoro iliyomo kwenye Kikanisa cha
Sistina na kuwa ni chemchemi inayobubujikia maisha mapya yanayojikita katika kazi
ya uumbaji na ukombozi.
Michoro hii ni kielelezo cha kazi ya Ukombozi; inaonesha
uhusiano kati ya Mwenyezi Mungu na Mwanadamu. Ni picha zinazodhihirisha: nguvu, utukufu
na ukuu wa Mungu katika kazi ya Uumbaji ambayo ni matunda ya uhuru kamili na upendo
wa dhati kabisa kutoka kwa Mwenyezi Mungu; inaunganisha mbingu na dunia. Kwa njia
ya Adamu, Mwenyezi Mungu anaanzisha uhusiano mpya na kazi ya Uumbaji, kwa vile mwanadamu
ameumbwa kwa sura na mfano wake, anakuwa na uhusiano wa moja kwa moja na Muumba wake.
Baba
Mtakatifu anasema, Msanii maarufu Michelangelo, baada ya miaka ishirini, aliweza kukamilisha
kazi hii kubwa inayoonesha Siku ya Hukumu, Yesu atakapokuja kuwahukumu wazima na wafu
na kwamba, Ufalme wake hautakuwa na mwisho.
Maadhimisho ya Masifu katika Kikanisa
cha Sistina kinachosheheni michoro mbali mbali ni kuonesha hija ambayo Mwenyezi Mungu
anaendelea kufanya na binadamu, changamoto kwa waamini kupaza sauti zao kwa Mwenyezi
Mungu: Muumbaji, Mkombozi na Hakimu wa wazima na wafu pamoja na zile za watakatifu
wote kwa kusema, Amina, Alleluiya.