2012-11-01 14:20:36

Kila mwamini anaitwa kuchuchumilia utakatifu, yaani maisha ya uzima wa milele katika utukufu wa Kristo


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika maadhimisho ya Sherehe ya Watakatifu Wote, Alhamisi, tarehe Mosi Novemba, 2012, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican, anasema hii ni Sherehe inayoonesha hija ya kihistoria inayopata utimilifu wa maisha yake kwa Mwenyezi Mungu.

Hiki ni kielelezo cha Kanisa linalosafiri katika nyakati na Kanisa ambalo tayari limekwishafikia utimilifu katika Yerusalemu ya mbinguni, ukweli unaojionesha katika umoja na watakatifu, hija ya maisha ambayo yalianza hapa duniani na hatimaye, kufikia hitimisho lake mbinguni.

Hapa duniani, Kanisa limeanzisha Fumbo la Umoja kwa kuwakusanya watu wote ili kuwapeleka kwa Mwenyezi Mungu, wakati huo huo, likishughulikia mshikamano na amani. Yesu aliteswa, akafa na kufufuka ili kuwaunganisha watoto wa Mungu waliotawanyika sehemu mbali mbali za dunia katika utume huu unaotekelezwa na Kanisa ambalo ni: Moja, Takatifu na Katoliki.

Wakristo ni sehemu ya Kanisa ambalo kimsingi linajifunua kwa ajili ya kudumisha umoja huu, ili kufikia maisha mapya yanayopata utimilifu wake mbinguni. Watakatifu ni watu ambao walijitahidi kuuishi ukweli huu, kwa njia ya Roho ya Kristo inayojidhihirisha katika Neno la Mungu na Sakramenti za Kanisa.

Ni watu wanaounganishwa na upendo kwa Kristo na Kanisa lake na hivyo kuwa kweli ni sura ya Mwana wa Mungu daima wakiendelea kutekeleza ule mpango wa Mungu wa kumuumba mwanadamu, kwa sura na mfano wake; ni umoja unaofumbata wote wanaounda Fumbo la Mwili wa Kristo katika umoja kamili.

Sherehe ya Watakatifu wote anasema Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, inawawezesha waamini kuonja maisha ya uzima wa milele wakiwa na mtazamo wa upendo wa Mungu na jirani, ili kwa pamoja kuweza kumfikia Mwenyezi Mungu na jirani. Kwa njia ya imani hii, waamini wote wanajawa matumaini ya kuwa ni watakatifu na hivyo kujiandaa kuadhimisha Siku ya Kuwakumbuka Marehemu wote, inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila mwaka ifikapo hapo tarehe 2 Novemba.

Katika maisha ya watakatifu, waamini wanaona ushindi wa upendo dhidi ya ubinafsi na kifo; wanachangamotishwa kumfuasa Kristo ambaye ni mlango wa maisha ya uzima wa milele na anatoa maana halisi ya maisha yanayosheheni upendo na matumaini.

Imani katika maisha ya uzima wa milele inawawezesha waamini anasema Baba Mtakatifu kupenda historia na hali ya maisha ya sasa bila ya kujishikamanisha na malimwengu, lakini katika uhuru kamili kwa kutambua kwamba, wao ni mahujaji wanaoipenda dunia, lakini moyo wao umejikita zaidi kwa mambo ya mbinguni.







All the contents on this site are copyrighted ©.