Rais Jakaya Kikwete akutana na kuzungumza na viongozi wa dini mkoani Kilimanjaro kuhusu
sakata la kinzani za kidini Tanzania
Viongozi wa dini mbali mbali katika Mkoa wa Kilimanjaro wameungana kuunga mkono jitihada
za Serikali kupambana na wanaharakati wa kidini ambao wanatumia dini kucheza siasa
kwa nia ya kuvuruga amani ya utulivu ambao umedumu nchini kwa miaka mingi.
Miongoni
mwa mambo mengine, viongozi hao wameitaka Serikali kuangalia upya sera ya usajili
wa taasisi za kidini nchini kwa nia ya kupunguza na hata kumaliza joto la uvunjivu
wa amani kwa kutumia mgongo wa dini.
Aidha, viongozi hao wameishauri Serikali
kuchukua hatua kali za kupambana na vitendo vya uvunjifu wa amani na utulivu kupitia
kisingizio cha dini ikiwa ni pamoja na kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya watu
wanaotumia mwanya wa dini kuingiza siasa katika dini na hivyo kuvunja amani.
Msimamo
huo wa viongozi wa dini umeelezwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa
Jakaya Mrisho Kikwete usiku wa Jumanne, Oktoba 30, 2012, wakati alipokutana na viongozi
hao ambao wamewasilisha matamko yao kwake katika shughuli fupi iliyofanyika Ikulu
Ndogo ya Mkoa wa Kilimanjaro mjini Moshi. Matamko hayo yanahusu vurugu za karibuni
katika Jiji la Dar es Salaam ambazo zilihusisha uvunjifu wa amani.
Viongozi
hao wakiongozwa na viongozi wao – Mwenyekiti wa Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata)
Mkoa wa Kilimanjaro Sheikh Ramadhan Salim, Sheikh wa Mkoa wa Kilimanjaro Sheikh Shaaban
Rashid na Maaskofu Glorius Shoo, Martin Shao na Isaac Amani wakiwasilisha madhehebu
ya Kikristo ya Wakatoliki, KKKT, Pentekoste na TAG na imani mbali mbali za dini ya
Kiislamu walifika Ikulu Ndogo kuwasilisha salamu kwa Rais Kikwete.
Ujumbe wa
viongozi hao ulifanana kabisa. Wote walilaani kudhalilishwa kwa Kitabu Kitakatifu
cha Quran kwa kukojolewa na kijana mmoja, kitendo ambacho kilisababisha kuvamiwa na
kuchomwa kwa makanisa ya Kikristo na kuibiwa kwa mali kutoka kwenye Makanisa hayo.
Baba
Askofu Martin Shao amemwambia Rais Kikwete: “Mheshimiwa Rais tumekuja kukusalimia
na kutoa tamko letu la kuunga mkono jitihada za Serikali yako katika kukabiliana na
uvunjifu wa amani kwa kisingizio cha dini kama ilivyodhihirika katika siku chache
zilizopita.”
Naye Sheikh Shaaban Rashid amemwambia Rais Kikwete: “Hatukubaliani
na mambo mawili, moja ni kunajisiwa kwa Kitabu Kitakatifu cha Mwenyezi Mungu cha Quran
na pili ni kuvunjwa na kuharibiwa kwa Nyumba za Ibada kama ilivyoonyeshwa katika matukio
ya Mbagala kule Dar es Salaam. Tunaunga msimamo wa Serikali yako katika kukabiliana
na mambo haya.”
Naye Mwenyekiti wa Bakwata katika Mkoa wa Kilimanjaro, Sheikh
Ramadhan Salim amemwambia Rais Kikwete: “Tumefadhaishwa na kitendo cha kunajisiwa
Kitabu cha Mungu – imepata kutokea pale Dodoma, imepata kutokea Boma Ng’ombe Mkoa
wa Kilimanjaro na sasa Mbagala, Dar es Salaam. Tunalaani pia vitendo vya kuvunja,
kuharibu na kuchoma moto nyumba za ibada.”
Ameongeza: “Tunaomba Serikali kuchukua
hatua tatu. Moja ni kuhakikisha kuwa hukumu ya uadilifu inafikiwa katika kesi zinazowakabili
waliohusika na vitendo hivi. Pili Serikali iangalie upya sera za uandikishaji wa taasisi
za kidini na tatu Serikali itoe msimamo kamili na sahihi kuhusu jambo hili badala
ya taarifa za matukio haya kutolewa na vyombo vya habari.”
Naye Askofu Martin
Fataely Shao amesema: “Tunasikitishwa na vitendo na matukio ya uvunjifu wa amani,
utulivu na mshikamano. Tunasikitishwa na kuibuka kwa vikundi vinavyodhalilisha dini
na imani ya watu wengine kwa kutumia vyombo vya habari na hasa redio. Hatukubaliani
na vitendo vya kukashifu dini na imani za watu wengine.”
Akizungumza katika
shughuli hiyo kwenye siku ya tatu ya ziara yake ya siku nne katika Mkoa wa Kilimanjaro,
Rais amewashukuru sana viongozi hao wa dini. “Leo nitalala usingizi mzuri kwa kuwa
mmetoa maneno ya kuponya nchi yetu. Nawapongezeni kwa uamuzi wa kukutana na kufikia
uamuzi huu.”
Rais Kikwete amesema kuwa kwa muda sasa amekuwa anaona dalili
za Tanzania kupelekwa pabaya siyo kwa tatizo la ukabila bali kwa tatizo la udini kwa
sababu ni dhahiri kuna watu hawafurahishwi na utulivu wa Tanzania na wangependa kuiona
Tanzania ikikumbwa na matatizo ya ukosefu wa amani na utulivu kama baadhi ya nchi
majirani.
Amesema kuwa ni dhahiri wako wanarahakati wa dini zote kubwa mbili
ambao wanatumia dini kujipenyeza katika ajenda za kisiasa na hivyo kuvuruga amani
na utulivu. “kazi ya wanaharakati hawa ni kukashifu dini za wenzao. Uzuri sheria za
nchi hii zinatosha kukabiliana na hali hii. Tunatoa uhuru wa watu kuabudu lakini hatutoi
uhuru wa watu kudhalilisha dini za watu wengine.”
Rais Kikwete amewahakikishia
viongozi hao wa dini kuwa Serikali yake haitalala katika kuhakikisha kuwa Tanzania
haiingii katika uvunjifu wa amani na utulivu kwa kisingizio cha dini. “Nataka kuwahakikishia
kuwa Serikali yenu iko macho. Kamwe, hatutaruhusu uvunjifu wa amani kwa kisingizio
cha dini. Nyie mmeonyesha mfano. Na sisi hatuwezi kuiachia nchi kutumbukia katika
matatizo.”