Nidhamu ya matumizi ya fedha na rasilimali ya umma ni lazima vipewe kipaumbele cha
kwanza!
Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican ifuatayo ni hotuba iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete
wa Tanzania wakati wa kufungua jengo jipya la ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu
za Serikali mkoani Kilimanjaro, hapo tarehe 30 Oktoba 2012.
Nakushukuru sana
Ndugu Ludovick Utouh kwa kunialika kuja kushiriki nanyi ufunguzi wa Jengo la Ofisi
ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali hapa Mkoani Kilimanjaro. Hii ni mara yangu
ya tatu katika kipindi kifupi kufungua majengo ya Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi. Mwaka
2009 nimefungua jengo la Singida. Mwezi Januari mwaka huu nilifungua jengo la Morogoro
na sasa nipo hapa Kilimanjaro kufanya kazi hiyo hiyo. Nimefurahi kuna majengo mengine
mawili katika Mikoa ya Lindi na Shinyanga ambayo nayo yamekamilika na yanasubiri kufunguliwa.
Napenda kuchukua nafasi hii kukupongeza sana wewe Ndugu Utouh na wafanyakazi
wote wa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi kwa kufanikisha ujenzi wa majengo haya. Hongereni
sana kwa kupiga hatua hii nzuri ya maendeleo. Endeleeni na kasi hii mpaka mtimize
ndoto yenu ya kuwa na ofisi zenu wenyewe kwenye kila Mkoa. Nakuahidi ushirikiano wangu
na msaada wa Serikali katika kila hatua mtakayopiga.
Mabibi na Mabwana; Sote
tuliopo hapa tunaridhika na jengo hili. Ni zuri, linapendeza na linapendezesha mandhari
ya Manispaa yetu ya Moshi. Limejengwa vizuri kwa ustadi mkubwa na kwa kuzingatia viwango
vya kimataifa. Natoa pongezi kwa wale wote walioshiriki katika kufanikisha ujenzi
wa jengo hili. Ninafurahi kusikia kuwa ujenzi wake umefanywa na kampuni za kizalendo
za J. S. Khambhaita Ltd ya hapa mjini Moshi, ikiwa mjenzi mkuu. Nawapongeza washauri
wasimamizi yaani ya Kampuni ya Space Link ikishirikiana na Digital Space Consultancy,
UNDI Consulting Group Ltd., na JB Costcare Consultant Ltd. Nawapongeza wote hao
kwa kazi nzuri ya kukamilisha ujenzi wa jengo hili kwa ustadi mkubwa.
Ndugu
Wafanyakazi wa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi; Naamini kukamilika kwa jengo hili
kunawapa faraja kubwa watumishi wa Ofisi ya Ukaguzi ya Mkoa wa Kilimanjaro kwa kuwa
mazingira yenu ya kufanyia kazi sasa yamekuwa mazuri. Lile tatizo la ninyi kufanya
kazi katika ofisi za kuazima sasa limekwisha. Kupatikana kwa jengo hili sasa kunawaondolea
mtihani wa kufanya kazi zenu kwenye ofisi za kupanga au za wale mnaotakiwa kuwakagua.
Sasa tunategemea kuwa mtatimiza ipasavyo wajibu wenu. Mtachapa kazi zaidi na kwa
uhuru zaidi.
Mabibi na Mabwana; Kwa ujumla, Serikali inatambua, kuthamini
na kuridhishwa na kazi ifanywayo na Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali
katika kusimamia nidhamu ya matumizi ya fedha na rasilimali za umma. Kazi yenu ni
nzuri na taifa linafaidi matunda yake. Uwajibikaji unazidi kuimarika katika Wizara
na Idara za serikali na umakini katika utunzaji na usimamizi wa rasilimali za umma
unaongezeka. Utendaji kazi ulio makini wa Ofisi hii umechangia katika kuleta mabadiliko
hayo.
Kwa kweli sina budi kuwapongeza kwa kazi nzuri mnayoifanya kwa manufaa
ya nchi yetu na maendeleo ya watu wake. Mnatoa mchango muhimu sana. Lakini, pamoja
na mafanikio hayo ya kutia moyo, bado tunayo kazi kubwa ya kufanya mbele yetu. Bado
kuna wizi, ubadhirifu na matumizi yasiyoridhisha ya fedha na rasilimali za Serikali.
Lazima muongeze juhudi zenu maradufu kupambana na changamoto hizo.
Mimi na
wenzangu Serikalini tunayo imani kubwa kuwa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi itaendelea na
kazi yake nzuri ya kuhakikisha kuwa rasilimali za taifa zinatumika vizuri kwa maslahi
ya taifa. Tuna imani kuwa mtazishinda changamoto zilizo mbele yenu. Naomba mfanye
kazi hiyo kwa umakini na weledi mkubwa. Kama mtu ni mwizi, hata awe kiongozi, anachezea
mali ya umma au ni mbadhirifu wa rasilimali za umma, basi achukuliwe hatua zinazostahili.
Hakika hii ndio njia pekee itakayowapa wananchi wote wa Tanzania fursa ya kufaidi
matunda ya uhuru na kuwapa maisha bora.
Ili kutimiza malengo haya maridhawa
hamna budi mfanye kazi kwa ushirikiano wa karibu sana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana
na Rushwa (TAKUKURU); Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) na Mkurugenzi wa Upelelezi wa
Makosa ya Jinai (DCI) pamoja na taasisi nyingine za Umma zinazofanya kazi katika eneo
hili.
Mabibi na Mabwana; Kwa upande wetu Serikalini tutakuwa bega kwa bega
na Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi. Kwenye hili hatutawaangusha. Serikali yetu inafuata
na kuheshimu utawala wa sheria. Hivyo hatutawaingilia katika utendaji wa kazi yenu.
Mtaendelea kuwa huru kama Katiba na Sheria inavyotaka muwe. Kazi kwenu, mshindwe
wenyewe! Pale mtapohitaji msaada tuambieni tutaangalia namna ya kuwasaidia.
Aidha,
Serikali itaendelea na mkakati wake wa kuboresha mazingira ya kufanyia kazi zenu na
maslahi ya wafanyakazi kila hali ya fedha itakavyoruhusu. Mahitaji ya Serikali ni
mengi na fedha tulizonazo hazitoshi lakini ninyi pia tutawapa umuhimu unaostahili.
Nawaomba muendelee kuongeza elimu na ujuzi wa wakaguzi wenu ili muweze kupambana na
changamoto za nyakati zinapojitokeza kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Kwa
ajili hiyo nimefurahi kusikia mnao mpango wa kujenga kituo cha mafunzo pale Gezaulole.
Jijini Dar es Salaam hilo ni wazo zuri sana na nawaomba mlitekeleze haraka. Jitahidini
kituo kiwe na hadhi ya kimataifa ili angalau kiweze kutoa mafunzo kwa maofisa wetu
na wenzetu wa nchi za jirani. Jambo hili linawezekana kabisa.
Mdhibiti na Mkaguzi
Mkuu wa Hesabu za Serikali; Wafanyakazi wa Ofisi ya Ukaguzi; Kabla sijamaliza
napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza sana kwa taasisi yenu kuchaguliwa kuwa Mjumbe
wa na Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa. Hii ni nafasi adimu na adhimu kwenu na
pia ni heshima kwa taifa letu. Kwa kuwa mmekwishaanza ukaguzi wa kimataifa, mkatuwakilishe
vizuri huko UN ili taifa letu liendelee kujizolea sifa kama ilivyo kawaida yetu. Nendeni
mkatimize wajibu wenu kwa mataifa yaliyotuamini, lakini pia tumieni nafasi hiyo kujenga
uwezo wa taasisi yetu na weledi wa wakaguzi wake. Ujuzi mtakaoupata huko utajenga
uwezo zaidi wa ukaguzi hapa nyumbani. Miaka sita sio michache, hivyo ninaamini wakaguzi
wengi watapata fursa ya kunufaika na fursa hiyo.
Mwisho naipongeza tena Ofisi
ya Taifa ya Ukaguzi kwa kupiga hatua hii kubwa ya kukamilisha jengo zuri la Ofisi
ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali katika mkoa wa Kilimanjaro. Kazi iliyobaki mbele
yenu ni kulitunza jengo lenu ili libaki kama linavyoonekana sasa kwa miaka mingi ijayo
na kufanya kazi kwa bidii zaidi, ufanisi zaidi na uhuru zaidi.
Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali; Wageni Waalikwa; Mabibi na Mabwana; Baada
ya kusema hayo sasa nipo tayari kufanya kazi iliyonileta hapa, kazi ya kufungua rasmi
jengo jipya la Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali, Mkoa wa Kilimanjaro.
Nawatakia kila la heri katika mwaka huu wa 2012.