2012-10-31 14:34:11

Maadhimisho ya Siku kuu ya Watakatifu Wote na Marehemu Wote yawawezeshe waamini kuwa kweli ni Mashahidi wa Upendo wa Mungu kwa watu wake!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumatano, tarehe 31 Oktoba 2012, katika katekesi yake kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, anasema kwamba: imani inapaswa kuwa ni sehemu ya undani wa maisha ya mtu: hii ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayomletea mwamini mabadiliko na utajiri mkubwa katika maisha ya kiroho.

Imani ni zawadi inayotolewa kwa njia ya Jumuiya ambayo ni Kanisa. Katika Ubatizo, mwamini anapokea zawadi ya imani na kuimwilisha katika maisha yake ya kila siku ndani ya Kanisa; imani ambayo kimsingi ni zawadi kwa mtu binafsi inajidhihirisha katika kusali Kanuni ya Imani na pale mwamini anaposhiriki kikamilifu katika maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anasema kwamba, hii ni chemchemi ya maisha mapya, inayomwezesha mwamini kwa njia ya Kristo na kwa kupitia Roho wake aliyempokea na kuendelea kuboreshwa kwa njia ya umoja ndani ya Kanisa. Kutokana na mwelekeo huu, Kanisa ni Mama ya Waamini, kama alivyowahi kusema Mtakatifu Cyprian kwamba, hakuna mtu anayeweza kujigamba kwamba Mwenyezi Mungu ni Baba yake bila kuzingatia kwamba, Kanisa ni Mama yake pia.

Ndani ya Kanisa kuna hifadhi kubwa ya Mapokeo Hai. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuhakikisha kwamba, wanakua na kukomaa katika misingi ya imani waliyoipokea kutoka kwa Mama Kanisa na kwa kuimwilisha katika uhalisia wa maisha, basi waamini hawa waweze kuwa kweli ni nuru ya mwanga wa Kristo na amani ya dunia.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ametumua fursa hii kutoa pole kwa wote walioathirika kutokana na kimbunga kilichoikumba Marekani katika siku za hivi karibuni na hivyo kusababisha maafa na uharibifu mkubwa wa mali na miundo mbinu. Baba Mtakatifu anapenda kuwahakikishia uwepo wake wa karibu kwa njia ya sala, hasa kipindi hiki kigumu cha historia ya maisha yao. Anapenda kuwatia moyo pamoja na kuwaonesha mshikamano wake wale wote wanaojishughulisha katika ukarabati na ujenzi mpya wa maeneo yaliyokumbwa na tufani hii.

Baba Mtakatifu amewatakia kheri na baraka mahujaji na wageni kutoka katika nchi zinazozungumza lugha ya Kiingereza waliohudhuria Katekesi yake siku ya Jumatano, lakini kwa namna ya pekee kabisa, mahujaji kutoka Nigeria wanaotembelea mji wa Roma kwa wakati huu.

Baba Mtakatifu pia ametumua fursa hii kwa ajili ya kuwashukuru waamini wote waliojibidisha kusali Rozari Takatifu wakati wa Mwezi Oktoba, uliotengwa maalum kwa ajili ya Rozari Takatifu, muhtasari wa maisha ya Yesu. Anawashukuru kwa kuwaombea Mababa wa Sinodi ya Maaskofu iliyohitimishwa hivi karibuni kama sehemu ya maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Maadhimisho ya Siku kuu ya Watakatifu wote pamoja na kumbu kumbu ya Marehemu Wote yawe ni matukio yatakawasaidia waamini kuwa mashahidi wa upendo wa Mungu.

Baba Mtakatifu anawapongeza Wanachama wa Umoja wa Vijana Wakatoliki Italia wanapoadhimisha miaka mia moja tangu umoja huu ulipoanzishwa kwa hakika, umekuwa na manufaa makubwa kwa Kanisa mahalia.

Baba Mtakatifu ametambua uwepo wa Wakuu wa Vyuo Vikuu na Taasi za Elimu ya Juu zinazosimamiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki wanaoendelea na mkutano wao hapa mjini Roma. Anasema, uwepo wao hapa Roma, ukuze imani yo kwa Kristo na Kanisa lake.







All the contents on this site are copyrighted ©.