Jumuiya ya Afrika Mashariki imepania kuimarisha mfumo wa ulinzi na usalama kwa nchi
wanachama!
Katika juhudi za kuimarisha mfumo wa ulinzi na usalama kikanda, Jumuiya ya Afrika
Mashariki (EAC) imeamua kukiimarisha kitengo chake cha utoaji taadhari na uwezo usuluhishi
wa migogoro, Shirika Huru la Habari la Afrika Mashariki (EANA) limeripoti.
Naibu
Katibu Mkuu wa EAC anayeshughulikia Shirikisho la Kisiasa, Dk Julius Rotich, alisema
hatua hiyo inatokana na kuwepo umuhimu mkubwa katika kufuatilia masuala yanayohusiana
na matunda yaliyopatikana kutokana na kuimarishwa kwa demokrasia, utawala bora, utawala
wa sheria na utetezi wa haki za binadamu na haki ya msingi ya uhuru. Aliyasema
hayo alipokuwa anafungua mkutano wa kitaalam wa siku tatu wa robo mwaka kati ya Umoja
wa Afrika(AU) na Jumuiya za Kiuchumi za Kikanda uliofanyika hivi karibuni jijini Arusha.
Mkutano huo ulijadili uendeshaji wa mfumo wa utoaji taadhari katika Afrika. “Mkutano
wenu unafanyika katika mazingira ya kuwepo ukuaji wa changamoto mpya katika ulinzi
na usalama katika kanda ya EAC. Ugaidi, usafirishaji haramu wa binadamu na madawa
ya kulevya, ukabila na vurugu katika jamii, migogoro ya kidini, uharamia na utakatishaji
fedha vinaongezeka katika kiwango cha kutisha,’’ Dk Rotich aliwaambia washiriki wa
mkutano huo. Aliongeza, “Madhara ya mabadiliko ya hali ya hewa na matokeo hasi
katika usalama wa chakula na uhaba wa rasilimali vinamchango wake katika picha hii
mbaya. Kazi yenu kwa pamoja na wadau wengine inategemewa kusaidia kuzuia madhara yanayotokana
na changamoto hizo.’’ Changamoto hizo, alisema, zimeongzeka kutokana na kuwepo
kwa Umoja wa Forodha na utekelezaji wa Itifaki ya Soko la Pamoja kuhakikisha kwamba
kunakuwapo na mwingiliano huru wa watu, kazi, huduma na mitaji na usalama wa uwekezaji
katika mipaka. Hata hivyo, changamoto za kiusalama hazipo katika Afrika Mashariki
pekee. “Bara hili katika miaka miwili iliyopita limejionea baadhi ya changamoto mbaya
zaidi za ulinzi na usalama, na zaidi katika ile inayojulikana ‘’ghasia zilizoibuka
katika nchi za Kiarabu,’’ Dk Rotich alisema. “Mgawanyiko na kusambaa kwa migogoro
hii na kujumuisha na madhara ya hali mbaya ya uchumi kimataifa, ni hofu mpya za ulinzi
na usalama zinazolikera bara la Afrika.” Malengo ya juhudi hizi zote ni kusadia
utoaji wa tahadhari,kuzuia migogoro ya ndani na baina ya nchi wananchama wa AU. Hii
ni mara ya pili EAC kuwa mwenyeji wa mkutano kama huo ambapo kwa mara ya kwanza ulifanyika
Aprili 2009.